Ukraine yasema Waafrika 1700 wanapigania Urusi
KYIV, UKRAINE
WIZARA ya Masuala ya Nje ya Ukraine imesema kuwa zaidi ya Waafrika 1,700 wanapigania Urusi kwenye vita vikali ambavyo vimekuwa vikiendelea kati ya nchi hizo mbili.
Andrii Sybiha, Waziri wa Masuala ya Nje wa Ukraine alisema Urusi inawashawishi Waafrika kwa kuwahadaa kuwa itawapa nafasi ya ajira kabla ya kuwaingiza vitani.
Sybiha alisema kuwa Ukraine imeanzisha mazungumzo na serikali za nchi mbalimbali Afrika ili kuzuia raia wao kutumiwa na Urusi vitani.
“Tunaona kwa njia ya wazi kwamba Urusi inajaribu kuwaingiza Waafrika kwenye vita hivi vikali ambavyo vimeishia katika maafa,” akasema Sybiha. Alikuwa akizungumza baada ya kukutana na Waziri wa Masuala ya Nje wa Ghana Samuel Okudzeto Ablakwa.
“Waafrika ambao wanapigania Urusi wanatoka nchi 36 kote bara hili,” akaongeza.
Ingawa hivyo, Urusi imekuwa ikikanusha kuwa inawasajili Waafrika jeshini kisha inawatumia kwenye vita kati yao na Ukraine.
Ablakwa alikiri kuwa Waafrika wanatumiwa na Urusi akasema sababu kuu ni kuhadaiwa kuwa watapata ajira na kuangukia utajiri.
“Wengi wao huwa hata hawafahamu chochote kwenye mafunzo ya kijeshi na hawajafunzwa. Walihadaiwa tu kisha sasa wanawekwa mbele wakati wa makabiliano,” akasema Ablakwa.
Waziri huyo alisema kuwa Ghana inasimama na Ukraine na kutoa wito kwa pande zote kusitisha vita hivyo ambavyo vimedumu kwa miaka minne.
Ablakwa aliongeza kuwa atazungumza na Rais wa Ukraine Volodymyr Zelenskiy awaachilie raia wawili wa Ghana ambao ni wafungwa wa kivita.
Wawili hao walinyakwa wakipigigania Urusi.
Ghana pia imesema itakuwa ikiendeleza mahamasisho kwa raia wake dhidi ya kuhadaiwa kusajiliwa kwenye jeshi la Urusi.