Ajabu miili 171 ikipatikana kwenye makaburi ya halaiki DRC
Haya yanajiri huku mapigano yakiendelea kushamiri licha ya makubaliano ya amani yaliyosimamiwa na Amerika.
Gavana wa jimbo la Kivu Kusini, Jean-Jacques Purusi, alisema kwamba maafisa waligundua makaburi mawili yenye jumla ya miili isiyopungua 171 katika vitongoji vya Kiromoni na Kavimvira, nje kidogo ya mji wa Uvira.
“Kwa sasa tumetambua maeneo mawili: kaburi moja la halaiki lenye takriban miili 30 huko Kiromoni, karibu na mpaka wa Burundi upande wa Congo, na lingine Kavimvira ambako miili 141 ilipatikana,” Purusi alisema kwa njia ya simu.
Maafisa wa shirika moja la kulinda la raia katika eneo hilo, walisema walitaka kutembelea makaburi hayo lakini walizuiwa na jeshi la Congo.
Naibu rais wa kundi hilo, Yves Ramadhani, alisema taarifa za awali zinaashiria waathiriwa waliuawa na waasi wa M23.
Gavana wa jimbo na wanaharakati hao wanadai kuwa waasi waliwaua watu hao kwa tuhuma za kushirikiana na jeshi la DRC au wanamgambo wanaounga mkono serikali.
Hata hivyo, pande zote jeshi la DRC na M23 zimewahi kushutumiwa kwa mauaji ya kiholela na ukiukaji wa haki za binadamu.
M23 ni kundi maarufu zaidi kati ya zaidi ya makundi 100 yenye silaha yanayowania ushawishi katika eneo la mashariki mwa DRC lenye utajiri wa madini karibu na mpaka wa Rwanda.
Mgogoro huo umeendelea kwa zaidi ya muongo mmoja na umechangia mzozo mkubwa wa kibinadamu, huku zaidi ya watu milioni saba wakitoroka makazi yao, kwa mujibu wa Umoja wa Mataifa.