Huzuni mvuvi akiuawa na mwingine kujeruhiwa na radi baharini
MVUVI mmoja alifariki na mwingine kujeruhiwa vibaya walipopigwa na radi wakivua samaki baharini katika eneo la Ingini, Lamu Jumamosi.
Kassim Badi Usama, 48, alifariki papo hapo ilhali mwenzake, Mohamed Wako, akiachwa na majeraha mabaya baada ya radi kuwachapa walipokuwa kwenye mashua yao wakivua huku mvua kubwa ikinyesha.
Kamanda wa Polisi kaunti ya Lamu, Bw Shadrack Ruto alithibitisha kisa hicho akisema mashua ya wavuvi hao, iliharibiwa kwa kupasuliwa na radi.
Bw Ruto aliwaomba wavuvi kuwa waangalifu na kupunguza shughuli zao baharini msimu huu wa mvua kubwa.
Meneja wa Kitengo cha Majanga na Uokozi (EOC Lamu Iftakkar Majid aliwasisitizia wavuvi, mabaharia na wakazi kuwa waangalifu msimu huu wa mvua kubwa ili kuepuka majanga zaidi.
Bw Majid aliwasihi kutafuta ushauri kutoka kwa kituo hicho cha majanga na pia idara ya hali ya hewa kabla ya kutekeleza shughuli zozote baharini.
“Pia ninawashauri wananchi kutotafuta hifadhi chini ya miti wakati kukinyesha kwani hilo huwaweka kwenye hatari ya kupigwa na radi,” akasema Bw Majid.
Wakati huo huo, familia ya mwendazake, inaiomba serikali kuwapa msaada kutokana na kuondokewa kwa mpendwa wao waliyemtaja kuwa tegemeo la kipekee.
Binamuye mwendazake, Bw Badi Nassir, alisema kakake ameacha mjane na watoto wawili.
“Binamu yangu ndiye tegemeo la familia yake. Mke na watoto wameachwa ukiwa. Serikali izingatie kuifidia familia ili angalau ijitegemee,” akasema Bw Nassir.
Mwenyekiti wa zamani wa Muungano wa Wavuvi (BMU) eneo la Faza ambako marehemu anatoka, Bw Mohamed Ali aliomba fedha za majanga zinazotengwa kila kukicha na serikali pia kuhakikisha zinawafikia wavuvi wa Lamu wanaokumbwa na majanga.