Iran: Kauli ya Trump kuhusu muafaka ni feki
TEHRAN, Iran
IRAN Jumanne iliendelea kuirushia Israeli makombora licha ya Rais Donald Trump kusema kuwa wameanza mazungumzo ya kusitisha vita Ukanda wa Mashariki ya Kati.
Israeli ilithibitisha kuwa ilishambuliwa ilhali Trump, Rais wa Amerika, alikuwa amesema kuwa kuna mazungumzo yanayoendelea na yamefikia hatua muhimu.
Maafisa wa ngazi ya juu kutoka Israeli ambao hawakutaka wanukuliwe na Reuters walisema kuwa Trump angependa sana vita hivyo visitishwe ingawa Iran nayo imekataa kabisa mazungumzo.
Mnamo Jumatatu, Iran ilisema hakuna mazungumzo ambayo yalikuwa yameandaliwa huku Afrika Kusini ikimkejeli Trump kutokana na madai yake kuwa anaweza kuwa kiongozi mpya wa kidini wa Iran na anaweza kudhibiti Mkondo wa Strait of Hormuz.
Waziri Mkuu wa Israeli, Benjamin Netanyahu, ambaye amekuwa mshirika wa karibu wa Trump jana alikuwa akitarajiwa kuandaa mazungumzo na maafisa wa usalama kuhusu nia ya Trump inayowasukuma waafikiane na Iran.
Ripoti kutoka Pakistan ziliarifu kuwa mazungumzo yanaweza kuanza mwaka huu.
Amerika-Israeli zilianza mazungumzo na Iran mnamo Februari 28 wakisema mazungumzo ya kushawishi Iran iachane na mpango wake wa kustawisha nyuklia yalikuwa yamefeli.
Hii ni licha ya Oman ambayo ilikuwa mpatanishi kwenye mazungumzo hayo kusema hatua kubwa ilikuwa imepigwa.
Vita hivyo vimeenea sana Ukanda wa Mashariki ya Kati.
Iran imekuwa ikishambulia nchi ambazo zina kambi za kijeshi za Amerika na pia kuharibu miundomsingi ya nchi hizo.
Pia imefunga njia muhimu ya kusafirisha mafuta ya Strait of Hormuz ambayo asilimia 20 ya mafuta ghafi hupitia.
Trump Jumatatu alisema alikuwa amesitisha mpango wa kushambulia viwanda vya nyuklia vya Iran ili nchi hiyo ifungue Mkondo wa Strait of Hormuz.
Hata hivyo, Iran nayo ilisema kuwa ipo tayari kwa makabiliano na itashambulia kambi za kijeshi na miundomsingi ya Amerika Ukanda wa Mashariki ya Kati.
“Hakuna mazungumzo ambayo yameandaliwa na Amerika na habari hizo ni feki kwa sababu wanalenga kudhibiti masoko ya mafuta. Kwa sasa Amerika-Israeli wamejipata pabaya zaidi kwenye vita hivi,” akasema Spika wa Bunge la Iran Mohammad Baqer Qalibaf.
Trump alikuwa amesema mazungumzo na Iran yalishirikisha Steve Witkoff na mkwe wake Jared Kusher ambao walikuwa kwenye mazungumzo ya hapo awali kabla ya vita kuanza.
Alisema mazungumzo hayo yalifanyika na afisa wa ngazi ya juu Iran mnamo Jumapili na Jumatatu.
Afisa mmoja kutoka Bara Ulaya alisema hakuna mazungumzo ambayo yalikuwa yamefanyika habari hizo zikithibitishwa na Misri, Pakistan na mataifa ya Gulf.