Hasara tele chai ya thamani ya Sh3 bilioni ikikwama kwa sababu ya vita Mashariki ya Kati
WAUZAJI wa bidhaa nje ya nchi wanaendelea kukadiria hasara kubwa huku bidhaa kama chai na kahawa zikikwama katika Bandari ya Mombasa na kwenye mabohari mbalimbali kote nchini.
Sekta ya chai ndiyo imeathirika zaidi, hali iliyosababisha hasara ya zaidi ya Sh 3.13bilioni baada ya kusitishwa kwa usafirishaji kwa muda wa takriban wiki tatu zilizopita kufuatia vita vinavyoendelea kati ya Israel, Amerika na Iran.
Mkurugenzi Mkuu wa Chama cha Biashara ya Chai Afrika Mashariki (EATTA), Bw George Omuga, alisema kila wiki sekta hiyo inapoteza kati ya kilo milioni 2 hadi 3 za chai zilizokusudiwa kusafirishwa kwenda Mashariki ya Kati.
Alieleza kuwa kufungwa kwa Mkondo wa Hormuz kumesababisha baadhi ya meli kufuta safari zao kuelekea Mombasa huku nyingine zikichelewa kutokana na kutumia njia mbadala ndefu zaidi.
“Tunasafirisha kati ya asilimia 20 hadi 25 ya chai yetu kwenda Mashariki ya Kati, lakini sasa soko hilo limeathirika vibaya kutokana na migogoro inayoendelea. Licha ya wafanyabiashara kununua chai, bado imehifadhiwa katika mabohari na Bandari ya Mombasa, ikiwa ni kati ya kilo milioni 8 hadi 10 za thamani ya zaidi ya Sh3 bilioni tangu vita vilipoanza,” alisema Bw Omuga.