DRC kupokea raia wake waliofurushwa na Trump Amerika
JAMHURI ya Kidemokrasia ya Congo (DRC) inasema inatarajia kupokea raia wa kigeni waliofurushwa kutoka Amerika chini ya makubaliano mapya na utawala wa Rais Donald Trump.
DRC itaanza kupokea watu hao mwezi huu, kulingana na taarifa iliyotolewa na Wizara ya Mawasiliano Jumapili, japo haikutoa idadi ya watu wanaotarajiwa kuwasili.
Ilielezea mpango huo kama wa “muda tu” na ambao unaashiria kujitolea kwa DRC “kuheshimu utu wa binadamu na umoja wa kimataifa”.
Kama sehemu ya mpango huo, Amerika itagharamia uhamisho wa raia hao wa kigeni na serikali ya DRC haitalipa gharama yoyote, taarifa hiyo ilisema.
Tangazo hilo lilijiri wakati ambapo utawala wa Trump unaendeleza juhudi za kupatanisha DRC na Rwanda na kuwezesha Amerika kufikia utajiri wa madini ulioko mashariki mwa DRC.
Amerika imesafirisha raia wa kigeni hadi mataifa ya Afrika kama vile Ghana, Cameroon, Equatorial Guinea na Eswatini, hatua ambayo imekosolewa na wanasheria na makundi ya kutetea haki za kibinadamu wakisema ni ukiukaji sheria.