Pope Leo: Simuogopi Trump, na nitaendelea kumponda
ALGIERS, Algeria:
PAPA Leo Jumatatu jioni alisema kuwa ataendelea kukemea vita licha ya kuvamiwa kwa maneno makali na Rais Donald Trump.
Akizungumza akiwa Algeria kwenye siku ya kwanza ya ziara yake Afrika, Papa Leo XVI ambaye ni kiongozi wa Kanisa Katoliki ulimwenguni alisema hawezi kunyamaza ilhali Ukristo ulikuwa ukitusiwa.
Papa Leo anaongoza zaidi ya wanachama bilioni 1.4 wa Kanisa Katoliki na atakuwa na ziara ya siku 10 barani Afrika katika mataifa mbalimbali.
“Sitaki kujibizana naye na sidhani kama neno la Mungu linastahili kutusiwa jinsi ambavyo baadhi ya watu wanavyofanya,” akasema Papa Leo.
“Nitaendelea kuzungumza kuhusu maovu ya vita, nihubiri amani na kuhakikisha mahali ambapo hakuna maelewano, watu wanazungumza ili kusaka suluhu,” akasema Papa Leo akizungumza Kiingereza.
“Watu wengi wanateseka duniani kutokana na vita na watu wengi wasiokuwa na hatia wanauawa. Lazima mtu asimame na kusema kuna njia bora zaidi ya kushughulikia masuala haya tata yanayogonganisha mataifa,” akaongeza.
Trump alimshambulia Papa Leo XVI kwa kupinga vita vya Amerika-Israel dhidi ya Iran na pia sera za Trump kuhusu uhamiaji.
“Papa Leo ni dhaifu katika kupambana na uhalifu na ana sera mbovu za kigeni,” Trump akachapisha kwenye ukumbi wake wa Truth Social.
Trump baadaye alitumia AI kuibuka na picha iliyomfananisha na Yesu na bendera ya Amerika lakini akaiondoa baadaye.