Trump ashindwa, apata faraja kwa kurefusha muda wa mazungumzo na Iran
WASHINGTON, Amerika:
RAIS wa Amerika Donald Trump jana alirefusha makubaliano ya kusitisha vita dhidi ya Iran ili kupisha mazungumzo zaidi ya amani.
Hatua ya Trump kulingana na taarifa yake ilichochewa na ombi la Pakistani ambayo imekuwa mpatanishi wake na Iran.
Hata hivyo, bado haijulikani iwapo Iran au Israel, ambayo ni mshirika wa Amerika kwenye vita hivyo, itakubali uamuzi huo wa Trump.
“Tumeamua kusitisha mashambulizi dhidi ya Iran hadi pale ambapo viongozi wao na wawakilishi wao watakuja na pendekezo la pamoja na mazungumzo yakamilishwe kwa njia moja au nyingine,”
Viongozi wa Pakistani wamekuwa mwenyeji wa mazungumzo ya amani ya kumaliza vita hivyo vilivyowaua maelfu ya raia.
Mazungumzo hayo yamekuwa yakifanyika Islamabad.
Hata alipokuwa akitangaza kusitishwa kwa vita, Trump alisema kuwa kwa meli za Amerika zitaendelea kuzima biashara za Iran kupitia uchukuzi wa majini.
Jana, bado maafisa wa ngazi ya juu katika serikali ya Iran hawakuwa wametuma taarifa iwapo wameridhia kauli ya Trump kuwa vita havitaendelea.
Duru kutoka Tehran zilisema Iran haikuwa imeomba muda huo wa kusitisha vita uongezwe kwa kuwa haja yao ni kulipua meli za Amerika ambazo zinazima biashara ya uchukuzi wa majini nchini humo.
Spika wa Bunge la Iran Mohammad Baqer Qalibaf alisema Iran bado inapima kauli ya Trump ambazo alisema ni za kuhadaa tu nchi hiyo kabla ya kushambuliwa tena.
Trump ameonekena kuwa ndumakuwili kwa kuwa majuma mawili yaliyopita alikuwa ametishia kuua kila mtu Iran. Wakati mwingine amekuwa akisema anamakinikia mazungumzo ili kumaliza vita kati ya Amerika-Israel na Iran.
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres ni kati ya viongozi ambao wameshutumu vitisho vya Trump na kusema sheria za kimataifa haziruhusu ukiukaji wa kibinadamu na mauaji ya raia.
Kauli ya Trump ya kurefusha mazungumzo hata hivyo inaonekana kama ushindi kwa Iran kwa kuwa inadhihirisha Amerika imeshindwa kulemaza nchi hiyo jinsi ilivyoahidi.
Amerika na Israel zilianza vita Februari 28 kwa mashambulizi ya anga dhidi ya Iran. Mzozo huo ulienea haraka hadi nchi za Ghuba zinazohifadhi kambi za kijeshi za Amerika na hadi Lebanon baada ya kundi la Hezbollah linaloungwa mkono na Iran kujiunga na vita.
Zaidi ya raia 5,000 wameuawa katika ukanda wa Mashariki huku maelfu wakitoroka makwao kwa hofu ya kushambuliwa Iran na Lebanon.