Hatari ya kukata rufaa kienyeji adhabu ikifanywa kali zaidi
KWA wengi wanaopatikana na hatia ya uhalifu, kukata rufaa huwa ni tumaini la kupata haki—njia ya kupunguza au kubatilisha adhabu wanayohisi si ya haki.
Hata hivyo, mchakato huu hauwafaidi kila mara. Katika baadhi ya visa, rufaa huleta adhabu kali zaidi, jambo linaloonyesha hatari iliyopo.
Daniel Njihia Miano alishtakiwa kwa kosa la wizi wa kutumia nguvu chini ya Kifungu cha 296(2) cha Kanuni ya Adhabu.
Ilidaiwa kuwa Septemba 11 2010 katika Kaunti ya Nyandarua, akiwa na wenzake, walimwibia Philip Karuoya Wambugu simu za mkononi huku wakiwa na mapanga na rungu.
Baada ya kusikilizwa kwa kesi, alihukumiwa kifungo cha miaka 14 jela.
Kwa kukosa kuridhika, Njihia alikata rufaa katika Mahakama Kuu ya Nakuru akipinga hukumu na adhabu.
Hata hivyo, upande wa mashtaka uliwasilisha notisi ya kuongeza adhabu, ukitaka apewe hukumu ya kifo.
Mahakama ilimweleza hatari hiyo kabla ya kusikiliza rufaa, lakini akaamua kuendelea nayo.
Mwishowe, Mahakama Kuu ilithibitisha hatia yake na kubadilisha kifungo cha miaka 14 hadi adhabu ya kifo. Rufaa yake ya pili katika Mahakama ya Rufaa ilitupiliwa mbali Machi 2026.
Katika kesi nyingine, Julius Kitsao Manyeso alihukumiwa kifungo cha maisha jela kwa ubakaji wa mtoto Malindi.
Mahakama ya Rufaa ilipunguza adhabu hiyo hadi miaka 40, lakini Serikali ilikata rufaa katika Mahakama ya Juu.
Mnamo Aprili 2025, mahakama hiyo iliamua kuwa Mahakama ya Rufaa ilikosea kisheria kubadilisha adhabu hiyo, na ikaamuru Manyeso aendelee kutumikia kifungo cha maisha.
SKS aliyepatikana na hatia ya kuwabaka mabinti zake wawili mwaka 2009, alihukumiwa miaka 50 jela kwa kila kosa.
Alipokata rufaa, Mahakama Kuu ilibadilisha adhabu hiyo kuwa kifungo cha maisha. Jaribio lake la baadaye la kutaka kesi ipitiwe upya lilikataliwa, licha ya mabinti wake kudai mashtaka yalikuwa ya kusingiziwa.
Kahindi Charo Masha aliyekuwa amehukumiwa miaka 15 kwa kumbaka msichana wa miaka 14, alikata rufaa na kuongezewa adhabu hadi miaka 20, huku Vincent Korir, aliyekuwa amehukumiwa miaka 25 kwa kumbaka mtoto wa miaka sita, akiongezewa adhabu hadi kifungo cha maisha baada ya rufaa yake kukataliwa.
Visa hivi vinaonyesha kuwa ingawa rufaa ni haki ya kisheria na njia ya kutafuta haki, inaweza pia kugeuka na kuwa na madhara makubwa zaidi kwa mshtakiwa.