Habari

TUKO KADI: IEBC yasajili wapiga kura wapya 1.87 milioni zoezi likielekea kukamilika

Na JUSTUS OCHIENG April 26th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

TUMEHuru ya Uchaguzi na Mipaka nchini (IEBC) imefikia takriban asilimia 75 ya lengo lake la kusajili wapigakura wapya, ikiwa imesajili watu milioni 1.87 kufikia sasa huku zoezi hilo likikaribia kukamilika.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa Aprili 24, tume hiyo ilisema kuwa jumla ya wapigakura wapya 1,876,274 wamesajiliwa tangu kuanza kwa zoezi hilo Machi 30, idadi inayoonyesha ongezeko kubwa kadri muda wa mwezi moja unavyokaribia kufikia mwisho.

Mwenyekiti wa IEBC, Erastus Ethekon, aliwahimiza Wakenya wanaostahili lakini bado hawajajisajili kufanya hivyo kabla ya zoezi kufungwa.

“Zimesalia siku nne pekee, tunawahimiza wananchi wote wanaostahili ambao bado hawajajisajili kutumia fursa hii kujisajili kama wapigakura,” alisema.

IEBC ilikuwa imeweka lengo la kusajili wapigakura wapya 2.5 milioni katika awamu hii, hatua inayolenga kupanua kwa kiasi kikubwa orodha ya wapigakura ikilinganishwa na ile ya uchaguzi wa 2022.

Tume hiyo ilisisitiza kuwa uhalali na uaminifu wa uchaguzi wowote hutegemea uwepo wa sajili sahihi na kamili ya wapigakura, ikieleza kuwa zoezi hilo linazingatia Kifungu cha 38 cha Katiba kinacholinda haki za kisiasa, ikiwemo kushiriki katika uchaguzi huru na wa haki.

Takwimu zinaonyesha kuwa Nairobi inaongoza kwa usajili wa wapigakura wapya zaidi ya 209,000, ikifuatiwa na Kiambu (97,557), Nakuru, (81,166) na Kakamega (80,711).

Kaunti nyingine zilizo na idadi kubwa ni Machakos (65,616), Bungoma (62,203) na Meru (56,486).

Hata hivyo, maeneo yenye ushiriki mdogo kihistoria kama Lamu na Isiolo yameripoti chini ya wapigakura 10,000 kila moja, kuonyesha tofauti zinazoendelea katika usajili wa wapigakura kote nchini.

Lamu imeongoza kwa idadi ndogo zaidi ya 8,345 huku Isiolo ikiwa na 9,291.

Katika eneo la Nyanza, usajili ulikuwa wa wastani huku kaunti ya Kisumu ikisajili wapigakura 37,090, Siaya 33,295, Homa Bay 39,770 na Migori 37,004.

Mbali na usajili mpya, IEBC ilisema kuwa wapigakura 159, 410 walihamisha vituo huku 2,817 wakirekebisha maelezo yao.

Tume hiyo pia ilihakikishia umma kuhusu uadilifu wa sajili ya wapigakura, ikieleza kuwa mfumo wa hatua kadhaa za uthibitishaji umetumika kuzuia udanganyifu na kurudiwa kwa majina.