Jamvi La Siasa

Atandi, Babu walumbana kuhusu mkutano wa Linda Mwananchi Kisumu

Na BENSON MATHEKA April 26th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

MBUNGE wa Alego Usonga, Sam Atandi, na mwenzake wa Embakasi Mashariki, Babu Owino, wametofautiana kuhusu mkutano wa vuguvugu la Linda Mwananchi unaopangwa kufanyika Kisumu leo.
Huku Atandi akisisitiza kwamba hautafanyika kwa kuwa wakazi hawaungi mkono mrengo huo, Owino anasema utafanyika hata wapinzani wao wakituma wahuni.
Akizungumza na mchanganuzi wa siasa Herman Manyora mnamo Alhamisi, Atandi alisema hakuna dalili kuwa wananchi wa Kisumu wana nia ya kuhudhuria mkutano huo.
“Kwanza kabisa hautafanyika kwa sababu…mkutano unafanyika tu ikiwa watu wa eneo hilo wanautaka,” alisema.
Alidai waandalizi wanapanga “kuagiza” vijana kutoka vyuo vya karibu kama Maseno ili kuonekana wako na umati.
“Hakuna mwananchi anayetaka kuhudhuria mkutano huo. Nilichoambiwa ni kwamba wanapanga kuleta wanafunzi kutoka vyuo mbalimbali. Watu wa Kisumu hawana hamu na mkutano huo,” akaongeza.
Hata hivyo, Babu Owino alithibitisha kuwa mkutano wao utafanyika Kisumu kama ilivyopangwa, akipuuza hofu ya kuvurugwa na wahuni.
Owino alisema hakuna vitisho vitazuia viongozi hao kushirikiana na wananchi na kujadili masuala muhimu ya kitaifa.
Alisisitiza kuwa Linda Mwananchi itaendelea kupigania haki na ustawi wa Wakenya ambao wanazidi kukumbana na changamoto sugu.
“Tukienda kwenye mkutano tunashambuliwa na wahuni, tusipoenda bado tunashambuliwa. Hata hivyo, tutaelekea Kisumu Jumapili, Aprili 26. Tunawakaribisha waje, sisi hatutaogopa,” alisema Owino.
Kauli yake inalenga kuondoa hofu miongoni mwa wafuasi wa vuguvugu hilo, huku akisisitiza mkutano huo utakuwa wa amani na kuheshimu sheria.
Pia alisihi wanaopanga kuzua vurugu kubadili msimamo wao.
Kauli ya Owino pia inajiri wakati mjadala mkali ukiendelea kuhusu mkutano huo, huku baadhi ya viongozi wakipinga na wengine kuunga mkono.
Licha ya mvutano waandalizi wamesisitiza kuwa wataendelea na mipango yao ya kuwasiliana na wananchi kote nchini.