Afya na Jamii

Wataalam waonya kuhusu bidhaa za kusafisha uke zilizokumbatiwa na wanawake wengi

Na MARY WANGARI April 30th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

SOKO la bidhaa za kutunza sehemu nyeti limeshika kasi katika miaka ya majuzi likijumuisha madai ya kupotosha yanayopigiwa debe na kusambazwa kupitia mitandao ya kijamii.

Bidhaa hizi awali zilijumuisha sabuni na vitambaa vya kusafisha na kupangusa sehemu nyeti ikiwemo vifaa vilivyodaiwa kuzuia viungo vya ukeni kulegea na kuviwezesha kushikamana zaidi.

Vifaa vya “kuyeyusha uke” vinavyojumuisha vipande vya mafuta ya nazi vinavyofanana na “tampons” vyenye muundo wa kuingizwa ukeni, ni miongoni mwa bidhaa mpya zilizozuka.

Bidhaa hizi za kisasa zinapigiwa debe kama nyenzo za “kujitunza nafsi,” zilizoundwa kutokana na malighafi asilia na zinazodumisha viwango mwafaka vya kemikali muhimu ukeni.

Zinasheheni manukato ya matunda anuai ikiwemo stroberi, cheri na pichi yanayosemekana “kuongeza harufu ya kuvutia ya matunda na unyevunyevu.”

Zinasifiwa kuwa zinahakikisha sehemu nyeti zinasalia safi na zenye harufu ya kuvutia kila siku.

Wataalam, hata hivyo, wametoa ilani kuhusu athari za bidhaa hizo wakionya kwamba zinaweza kuvuruga kemikali asilia ukeni inayokinga maambukizi, kuzidisha mwasho na mzio.

Bidhaa hizo zinasheheni mafuta na kemikali za kuzihifadhi zinazosababisha matatizo kiafya zinapotumiwa ukeni.

Wataalam wanasisitiza umuhimu wa kuosha sehemu nyeti kwa maji safi na bidhaa zisizo sheheni manukato, wakifafanua kwamba uke una uwezo wa kujisafisha wenyewe pasipo kuhitaji kuoshwa kutoka ndani wala manukato.

Harufu ya uke ni kawaida na inaweza kubadilika kwenye vipindi vya hedhi.

Hata hivyo, wauzaji bidhaa hizi husisitiza dhana kwamba harufu asilia ya ukeni inachukiza.

“Bidhaa inaponuiza kwamba mwili wako unahitaji kuwa na harufu ya matunda ili ukubalike, haisuluhishi suala la matibabu, inaunda tatizo la kijamii,” wanafafanua wataalam.

Bidhaa nyingi yamkini hutegemea hofu ya wanawake kuhusu harufu asilia.

“Muundo wa biashara hii yamkini unategemea, kwa sehemu fulani, wanawake kuhofia harufu asilia ya sehemu nyeti zao,” wanasema wataalam.

‘Mabadiliko asilia ya harufu ni sifa ya kawaida kibayolojia na haihitaji kufunikwa.”
Aidha, viungo vya mafuta vinavyotumiwa katika baadhi ya bidhaa za ukeni zinaweza kudhoofisha kondomu na kuzidisha tishio la kupasuka na mimba zisizotarajiwa.