Kimataifa

Wagonjwa wa Ukimwi wahepa matibabu kwa hofu ya kushukiwa kushiriki ushoga

Na REUTERS May 1st, 2026 Kusoma ni dakika: 2

DAKAR, Senegal:

IMEBAINIKA kuwa wagonjwa wachache wanatembelea vituo vya kupima maambukizi ya Ukimwi kutokana na kamatakamata zinazolenga mashoga Senegal.

Maafisa wa Sekta ya Afya pamoja na data ya serikali zilizoonwa na Reuters zinathibitisha hilo na kuweka taifa hilo pabaya kuhusiana na vita dhidi ya maambukizi ya Ukimwi.

Mwezi uliopita, Senegal ambako ushoga umeharamishwa, iliongeza hukumu ya kufungwa jela kwa wapenzi wa jinsia moja hadi miaka 10.

Pia ilichukua hatua na kuharamisha mahamasisho yanayoeneza ushoga.

Haya hayakutosha huku Senegal ikiongeza faini kwa wanaohusika na ushoga hadi Sh3.157 milioni.

Kwa mujibu wa mashirika ya kupigania haki na vyombo vya habari, watu 86 wamekamatwa kwenye oparesheni ambayo ilianza mnamo Februari.

Wakati huo, utawala wa Rais Bassirou Diomaye Faye ulikuwa ukijiandaa kuwasilisha mswada mpya dhidi ya ushoga bungeni.

Kamatakamata hizo zinajumuisha watu 18 ambao walinyakwa mnamo Aprili 19 eneo la Linguere, kilomita 300 kutoka Dakar.

Chini ya sheria hii mpya, watu wawili waliopatikana kuwa mashoga wamehukumiwa gerezani kwa makosa ya kuambukizana virusi vya ukimwi.

Takwimu kutoka Baraza la Kitaifa la Kupambana na Ukimwi Senegal zinaonyesha kuwa wagonjwa wanahepa kuendea dawa ambazo zinatibu na kulemaza HIV, kutokana na hofu ya kukamatwa.

Baadhi ya vyombo vya habari navyo vimehatarisha maisha ya wanaokamatwa kwa kuchapisha majina yao na hali yao ya ukimwi.

“Huu ni mwenendo ambao haukubaliki kwa sababu unahatarisha maisha ya watu,” akasema Dkt Safiatou Thiam, ambaye alikuwa waziri wa zamani wa Afya.

“Ni wazi kuwa kamatakamata hizi za serikali zitaathiri kazi yetu ya kuendeleza vita dhidi ya ugonjwa huu,” akaongeza akitaka hali ya wagonjwa iwekwe siri jinsi ambavyo wahudumu wa afya wamekuwa wakifanya wakitekeleza wajibu wao.

Kwa mujibu wa Shirika la Kimataifa la UNAIDS, Senegal ni kati ya mataifa manne Magharibi na Kati mwa Afrika ambako kumekuwa na ongezeko la maambukizi mapya ya ukimwi.

Baadhi ya wahudumu wa afya pia waliweka wazi kuwa walikuwa wametishwa wakitekeleza wajibu wao na sasa hawapimi wagonjwa.