Boma za kifahari zinazotumiwa kusuka dili kali za siasa
Nyuma ya kuta ndefu, milango yenye ulinzi mkali na orodha maalum za wageni, baadhi ya maamuzi makubwa zaidi ya kisiasa nchini Kenya huzaliwa mbali na macho ya umma.
Katika makazi ya kifahari yaliyofichika kwenye vitongoji vya kama Karen, Runda, Muthaiga na Lavington, pamoja na maeneo mengine ya nguvu za kisiasa nchini, mikakati hupangwa kwa kina, mahasimu hupunguzwa makali, na miungano ya kisiasa huundwa kabla haijatangazwa hadharani kupitia mikutano ya kampeni au taarifa rasmi za vyama.
Nyumba hizi—zinazomilikiwa na wanasiasa wakuu, wapangaji wa siasa, wafanyabiashara wenye ushawishi na wapatanishi wa kisiasa—zimekuwa kwa miaka mingi vituo visivyo rasmi vya maamuzi vinavyobeba mwelekeo wa siasa za taifa.
Ni katika mazingira haya ya faragha ambapo pande hasimu hukutana kwa mazungumzo ya moja kwa moja, bila kamera, bila mikutano ya hadhara na bila shinikizo za wanachama wa vyama au mirengo ya kisiasa.
Vyanzo vya karibu na mikutano hii vinaeleza kuwa mazingira ya nyumbani huruhusu mazungumzo ya wazi zaidi. Msimamo wa kila upande hupimwa kwa utulivu, maafikiano hutafutwa kwa upole, na mipaka huwekewa bila hofu ya madhara ya kisiasa ya haraka au taarifa kuvujwa kwa umma.
Matokeo ya mikutano hii mara nyingi huwa ni msimamo wa kisiasa unaotangazwa hadharani lakini uliosukwa kwa siri nyuma ya pazia la mazungumzo marefu, ya usiku na wakati mwingine ya siri kubwa.
Hata hivyo, kutegemea nyumba binafsi kama vituo vya mazungumzo ya kisiasa kumeibua mjadala mkali kuhusu uwazi, uwajibikaji na afya ya demokrasia nchini Kenya.
Wapo wanaoamini kuwa mazungumzo ya aina hiyo ni muhimu kuvunja mkwamo wa kisiasa, hasa pale taasisi rasmi zinaposhindwa kufikia makubaliano. Lakini wakosoaji wanaonya kuwa mwelekeo huu unahimiza maamuzi ya wasomi wachache, wakiacha wananchi na taasisi za kidemokrasia nje ya mchakato muhimu wa uamuzi.
Kenya inavyokaribia uchaguzi mkuu ujao, nyumba hizi tena zinatarajiwa kuwa maeneo ya mazungumzo ya kimya yatakayobeba hatima ya siasa za taifa.
Kiongozi wa Chama cha Safina, Jimi Wanjigi, ambaye pia ni mfanyabiashara na mwanasiasa, ni mmoja wa watu wanaoelewa kwa kina mazungumzo ya nyuma ya pazia.
Anasema mikutano hiyo haihusu siasa za kawaida za majukwaani bali maamuzi ya juu kabisa ya mamlaka.
“Mikutano ya nyuma ya pazia haihusu kitu kingine isipokuwa urais. Haipigiwi kelele wala kutangazwa. Ukiona picha mtandaoni, ni maigizo tu,” alisema.
Wanjigi anakumbukwa kama mmoja wa wahusika muhimu katika uchaguzi wa 2013, ambapo alihusika katika mikakati ya ndani ya muungano wa Jubilee ulioleta pamoja Uhuru Kenyatta na William Ruto.
Kwa mujibu wa watu waliokuwa karibu na mchakato huo, alisaidia kuunda mtandao wa kisiasa uliounganisha vyama, kupanga rasilimali na kuimarisha mikakati ya kampeni ya mashinani.
Rais William Ruto mwenyewe amewahi kuthibitisha kuwa makubaliano ya 2013 kati yake na Rais mstaafu Uhuru Kenyatta yalifanyika katika nyumba ya Wanjigi mtaani Muthaiga, akimtaja kama mhusika muhimu katika mchakato huo.
Wanjigi anasema mikutano hiyo ilibaki siri kwa miaka mingi hadi 2017 walipoachana kisiasa.
“Tulibadilisha siasa za nchi ndani ya nyumba yangu. Hakuna aliyefahamu kilichokuwa kinaendelea hadi tulipotofautiana kisiasa,” alisema.
Leo, nyumba za wanasiasa wakuu kama Uhuru Kenyatta, marehemu Raila Odinga, Musalia Mudavadi, Kalonzo Musyoka, na hata viongozi wa vyama kama Francis Atwoli na Timothy Bosire zimeendelea kuwa sehemu ya mazungumzo ya kisiasa.
Nyumba hizi pia zimekuwa sehemu ya mikutano ya kimkakati inayohusisha wafanyabiashara wakubwa, viongozi wa taasisi za fedha na wapangaji wa siasa kutoka maeneo mbalimbali ya nchi.
Wachambuzi wa siasa wanasema nyumba hizi zimekuwa “vyumba vya maamuzi” ambapo miungano huundwa, nafasi za uongozi hugawanywa na mustakabali wa siasa hupangwa kabla ya wananchi kufahamu kinachoendelea.
Profesa Gitile Naituli wa Chuo Kikuu cha Multimedia anaeleza kuwa siri na usalama ndizo sababu kuu zinazofanya viongozi kupendelea mikutano ya aina hiyo.
“Nyumbani hakuna udukuzi, hakuna kamera, na hakuna uwezekano mkubwa wa taarifa kuvujwa. Unajua kila mtu aliye ndani na unadhibiti mazingira yote ya mazungumzo,” anasema.
Hata hivyo, wakosoaji wanasema kuwa maamuzi ya kitaifa yanapofanywa kwa njia hii ya siri, wananchi huachwa nje ya mchakato wa kidemokrasia ambao unapaswa kuwa wazi na shirikishi.
Kumekuwa na mifano mingi ya mikutano kama hiyo katika historia ya kisiasa ya Kenya. Kabla ya uchaguzi wa 2022, miungano kama Kenya Kwanza na Azimio iliundwa kupitia mazungumzo ya kina yaliyofanyika katika nyumba za viongozi mbalimbali jijini Nairobi.
Uchaguzi wa 2027 unavyokaribia, nyumba hizi zimeanza tena kuonekana kama maeneo ya mikutano ya kimkakati. Vyanzo vinaeleza kuwa tayari kuna mikutano kadhaa ya ngazi ya juu iliyofanyika katika makazi ya Karen na Runda, ikihusisha viongozi wa upinzani wanaojaribu kusuka muungano mpya dhidi ya serikali ya sasa.