Mashairi

USHAIRI: Uhuru ni kiongozi

May 7th, 2026 Kusoma ni dakika: 5

Uhuru wa Kenyataa, liweza tenda makuu,
Taifa weza kung’aa, nchi piga hatua kuu,
Mambo yenye umang’aa, ‘liisha kwa njia kuu,
Uhuru ni kiongozi, alitenda mema nchini.

Watahiniwa kuweza, lipiwa za mitihani.
Hilo jambo ‘liongeza, walofanya mutihani,
Alisaida punguza, mzigo kwa wazazini,
Uhuru ni kiongozi, alitenda mema nchini.

Gharama karo shuleni, iliweza kupungua,
Uhuru alifanyeni, milango heri fungua,
Elimu ya Kenya nchini, ‘liweza vizuri kua,
Uhuru ni kiongozi, alitenda mema nchini.

Katika miundombinu, barabara weza jengwa,
Barabara kawa tunu, kwa njia zilimopangwa,
Barabara wekwa winu, katoa sura ya jangwa,
Uhuru ni kiongozi, alitenda mema nchini.

Kajenga reli kisasa, toka pwani hadi bara,
Nchi ikawa na usasa, pamoja na nzuri sura,
Ujenzi wenye kisasa, ulifanya Kenya bora,
Uhuru ni kiongozi, alitenda mema nchini.

Usambazaji wa stima, uliweza wekwa nchini,

Akina baba na mama, wakapanda toka chini,
Umeme ni nguzo kama, weza inua wa chini,
Uhuru ni kiongozi, alitenda mema nchini.

Kwa wizara ya afya, bima ilikuwa nzuri,
Linda mama ya afya, ‘kajifungua vizuri,
Wanafunzi na afya, ‘liwalinda njia nzuri,
Uhuru ni kiongozi, alitenda mema nchini.

Vituo vyenye huduma, vilirahisisha mambo,
Wananchi pata huduma, nchi ikawa nzuri umbo,
Vitambulisho huduma, shika kwa rahisi jambo,
Uhuru ni kiongozi, alitenda mema nchini.

Aliazima umoja, miongoni mwa wakenya,
Alitaka Kenya moja, kwa kunganisha wakenya,
Wananchi wawe wamoja, kwenye taifa la Kenya,
Uhuru ni kiongozi, alitenda mema nchini.

Na aliweza ungana, wa siasa mahasimu,
Ili anza kupambana, uongozi wa kuzimu,
Aliweza kupangana, na vongozi nchini humu,
Uhuru ni kiongozi, alitenda mema nchini.
JOSHUA OMACHE,
CHUO KIKUU CHA KIBABII

Bubu Kunena

Mbona mnakunja sura, mlijua mwisho wake?
Naona imewakera, bubu kupata la kwake,
Si siri mwagaragara, na mito kupiga teke,
Kwani bubu akinena, ni baraka au bina?

Katu haiwezekani, wengine wamechangia,
Bubu tu anene nini, mjadala ‘kaingia,
Kwani hawana imani, hata ya kujitungia?
Kwani bubu akinena, ni baraka au bina?

Wengine washangilia, Wakosatonge na bubu,
Mwanga ‘mewamulikia, katika giza na tabu,
Ni baraka kwao pia, bubu kuwapa majibu,
Kwani bubu akinena, ni baraka au bina?

Mfisadi na pwaguzi, ni bina wameambiwa,
‘Mevunjika zao ngazi, siri zinafichuliwa,
Ujanja wao wa juzi, bubu sasa atongowa,
Kwani bubu akinena, ni baraka au bina?

Bubu sasa u motoni, kashikwa na wenye siri,
Roho yake mkononi, hukumu akisubiri,
Kumbe kunena ni shani, kunena kumbe shubiri,
Kwani bubu akinena, ni baraka au bina?

Mwacheni aseme lake, mwacheni amwaye yote,
Lilo’funga moyo wake, mara moja alikate,
Wano’cheka na wacheke, wano’teta na watete,
Kwani bubu akinena, ni baraka au bina?
AUSTINE O ONYANGO
‘MALENGA WA MTO NILE’
CHUO KIKUU CHA JARAMOGI (JOOUST)

Bei ya mafuta

Mafuta yamepanda, kama mwewe angani,
Bei imekuwa kubwa, haina hata thamani,
Mifuko ina mashimo, imetoboka jamani,
Gari sasa ni sanamu, limebaki uwanjani.

Nakwenda kituoni sasa, na hofu tele moyoni,
Gharama zinanitesa, nina huzuni jamani,
Kila siku ni mkasa, mfuko hauna nguvu,
Gari sasa ni sanamu, limebaki uwanjani.

Mshahara hautoshi, lita mbili ni gharama,
Maisha hayashikiki, tunabaki kusononeka,
Hata safari hazikwendi, tunabaki tumerama,
Gari sasa ni sanamu, limebaki uwanjani.

Barabara ziko wazi, magari yamepungua,
Kupaki ndiyo uamuzi, jua likituchoma,
Hali hii ni dhiki kuu, kamba inatubana,
Gari sasa ni sanamu, limebaki uwanjani.

Enyi wenye mamlaka, tazameni hali yetu,
Mioyo imechoka sana, kipato ni duni kwetu,
Bei ishuke haraka, ipone mitambo yetu,
Gari sasa ni sanamu, limebaki uwanjani.

Hatima nafunga tamati, kwa kilio na huzuni,
Maisha yanatuyumba, tunaishi kwa huzuni,
Tunaomba bei ishuke, turudi barabarani,
Gari sasa ni sanamu, limebaki uwanjani.
DENNIS KIOKO
‘MHARIRI CHIPUKIZI’
CHUO KIKUU CHA KITEKNOLOJIA CHA MURANG’A

Wavyele nambie

Machozi yatirirka, huzuni na sikitiko
Moyoni nasikitika, huzuni mnijazako
Watoto wadogo kuoleka, wapata jiko
Wavyele wangu mnambie, haya maisha gani?

Sikilizeni makini, ushauri mpewapo
Shule zipo likizoni, wanenu wapoteapo
Wazazi mwanyamazani, wenu waharibikapo?
Wavyele wangu mnambie, haya maisha gani?

Swali niliulizalo, jibu lake silipati
Kote jini nilizungukalo, jibu silipati
Somo liirudiwalo, wanafunzi hawapati
Wavyele wangu mnambie, haya maisha gani?

Shule zifunguliapo, wako wapi wanafunzi?
Darasani wafikapo, hakunako wanafunzi
Wamekuwa wakifiapo, kidondani kama nzi
Wavyele wangu mnambie, haya maisha gani?

Nasaha mwaziweka mbali, watoto hamwapi
Hawatulii kwenye Manzili, wangali kutapi
Wamekuwa tapeli, moyo wenu haumpapi
Wavyele wangu mnambie, haya maisha gani?

Fumbueni macho yenu, mwangalie siku kesho
Wakilalamika wenu, hawaangalii kesho
Mwajiaribia yenu, hakuna wetu wa kesho
Wavyele wangu mnambie, haya maisha gani?

Tamati nafikia, wazazi na watoto wenu
Ningali nalalamikia, usalama wa wenu
Mashauri mwafukia, hawahitaji wanenu?
Wavyele wangu mnambie, haya maisha gani?
ROMANO NDUYO

Nimekombolewa

Nimekuwa kanisani, kumuomba Mungu wangu
Na sadaka mfukoni, kushukuru Mungu wangu
Nikatia kikapuni, fungu la kipato changu
Leo nimefunguliwa, Mimi si mfungwa tena!

Mimi si mfungwa tena, zimefutwa dhambi zangu
Nimetubu kwa kunena, kumweleza Mungu wangu
Nikaomba kufanana, na Yesu Mwokozi wangu
Leo nimefunguliwa, sitotenda dhambi tena

Sitotenda dhambi tena, siendelei kutusi
Nitakoma kupigana, iniondoke mikosi
Nimezivunja laana, tena sina wasiwasi
Leo nimefunguliwa, nikawa kiumbe mpya

Nikawa kiumbe kipya, sitaki tena kulewa
Nikapewa mwili mpya, dhambini kukombolewa
Nikajazwa nguvu mpya, na pia kubarikiwa
Leo nimefunguliwa, Mimi nimebadilika!

Nifikapo ukingoni, natua yalo moyoni
Nawaombea wendani, pia mtoke dhambini
Mmwondokee shetani, Mungu awasameheni
Mimi nilitubu kwake, akanipa msamaha
JAPHETH NZOMO
‘ZAO LA HEKIMA’
CHAKIMUT

Saa ya bosi

Siku yangu imeisha, ni salama salimini
Usiku wote ‘mekesha, hapa kwetu kituoni
Sare nimezirudisha, niende zangu nyumbani
Ni masaa ya bosi, brigedia anafika

Ni masaa ya bosi, brigedia anafika
Leo hataki matusi, wallahi mebadilika
Menilipia teksi, mwenzenu ninashtuka
Bosi amekuwa mwema, wallahi siamini

Bosi amekuwa mwema, wallahi siamini
Leo anipa heshima, mimi nashindwa kwa nini
Kapenda yangu huduma, au kenda msikitini

Wacha nifike nyumbani, kesho tajua ukweli

Wacha nifike nyumbani, kesho tajua ukweli
Nimejilaza kochini, nabishana na akili
Mesegi ipo simuni, menitumia nauli
Nifike zamu kazini, ataka kwenda shughuli

Nifike zamu kazini, ataka kwenda shughuli
Amenipa usukani, na kibandani silali
Ninajihisi ndotoni, machweo anawasili
Naenda zangu nyumbani, anaingia zamuni

Naenda zangu nyumbani, anaingia zamuni
Leo silali kochini, naenda zangu bedini
Macho yangu siamini, pengine nipo ndotoni
Hii saa yake bosi, kwangu yafanya nini?

Hii saa yake bosi, kwangu yafanya nini?
Ni saa ya almasi, limewekwa beserani
Mjinga ninajihisi, mambo haya mambo gani?
Mke wangu namuita, upesi aja chumbani

Mke wangu namuita, upesi aja chumbani
Moyo wangu wanitweta, saa ipo mkononi
Kuona kajikunyata, kazirai sakafuni
Niko na yeye wodini, apone anipe jibu
EZEKIEL NZEKE
‘USTADH KARMA’
MURANG’A

Niombeeni

Kwa nudhuma naandika, chozi likitiririka,
Nguvu zinanikatika, na mwili kutetemeka,
Ukweli usokanika, maini unaokata,
Sitaki mulielie, niombeeni mwenzenu.

Mtima wanishituka, kila ninapokumbuka,
Kwamba siku itafika, duniani kupatoka,
Nirudi kwake Rabuka, ulimwengu kuutoka,
Wala msilielie, niombeeni mwenzenu,

Siku itakapofika, roho yangu ikang’oka,
Muache kuweweseka, machozi yakawatoka,
Nifunikeni haraka, mwilini kusitirika,
Kamwe msilielie, niombeeni mwenzenu.

Ndugu nanyi kina kaka, mikono mujenishika,
msije nje kutoka, mabaya yakanifika,
Muilinde yangu shuka, hadi masaa kufika,
Wala msilielie, muniombee mwenzenu.

Sitawa na mamlaka, ya kuswali kwa hakika,
Basi mutakaofika, muniombee baraka,
Nende ikuta fanaka, ya dua zenu kifika,
Yani msilielie , muniombee mwenzenu.

Kisha msiche kutoka, nyumbani kwenu kufika,
Riziki mwendeisaka, na mengine kadhalika,
Uwaondoke wahaka, kiwewe kuwaepuka,
Tena msilielie, muniombee mwenzenu.

Na wakwangu wahibaka, wazazi na kina kaka,
Kina dada mewatoka, aushi mekamilika,
Munitolee na zaka, naimani itafika,
Jama msilielie, muniombee mwenzenu.
SALIM MWASUNA
‘MWASUNA MSHAIRI’
KWALE

Mwambieni Shangazi!

Mwambieni shangazi, salamu nimemtumia,
Kila kucha na machweo, moyo alinichukia,
Alitamani tuanguke, huzuni itutawale,
Kwa mkono wa Mungu, mafanikio yametimia,
Mungu amenisaidia, mafanikio yamefika.

Kwa hila na fitina, njama alizozipanga,

Akataka tushindwe, maisha yawe matanga,
Lakini nuru ya Mola, gizani ikaangaza,
Kwa neema ya Mwenyezi, tumefanikiwa sana,
Mungu amenisaidia, mafanikio yamefika.

Alitaka tuwe duni, tuishi kwa shida na dhiki,
Tuonekane wa chini, tukose hata marafiki,
Lakini Mungu wa haki, ametupa ushindi,
Leo tunasimama imara, kwa rehema zake tele,
Mungu amenisaidia, mafanikio yamefika.

Mwambieni shangazi, wivu si njia ya heri,
Moyo wa husuda, haujengi kesho njema,
Mungu ndiye mgawaji, riziki na kila kheri,
Nami ameninyanyua, akanitoa pabaya sana,
Mungu amenisaidia, mafanikio yamefika.

Leo nyumba imesimama, na watoto wasoma,
Baraka zimeongezeka, kwa rehema zisizokoma,
Si kwa nguvu zangu, wala akili za binadamu,
Ni Mungu aliyefanya, jina lake litukuzwe daima,
Mungu amenisaidia, mafanikio yamefika.

Sitetemeshwi na maneno, wala vitisho vya watu,
Nina ulinzi wa Mola, siogopi wala katu,
Mwambieni kwa heshima, safari si bahati
Ni Mungu amenifikisha, kwenye ushindi wa haki,
Mungu amenisaidia, mafanikio yamefika.

DENNIS KIOKO
‘MHARIRI CHIPUKIZI’
CHUO KIKUU CHA KITEKNOLOJIA CHA MURANG’A