Joho ataka mkataba kwanza na Ruto ndio aanze kuvumisha ‘Tutam’
WAZIRI wa Madini na Uchumi wa Baharini, Bw Hassan Joho, ametangaza sharti la mkataba wa kisiasa kati yake na Rais William Ruto, ili amuunge mkono kwa awamu ya pili ya uongozi 2027.
Akizungumza katika mkutano wa kisiasa Kwale, Bw Joho alisema kuwa mkataba huo utahakikisha kwamba baada ya Rais Ruto kukamilisha mihula yake miwili, ataunga mkono eneo la Pwani kuwania urais mwaka wa 2032.
Waziri huyo alisema mkataba anaoutaka na Rais Ruto ni wa urithi wa kiti cha urais baada ya uchaguzi mkuu ujao, akisisitiza nia yake ya kuwania urais na kuwataka Wapwani kumuunga mkono.
“Tutamuunga Rais Ruto kwenye uchaguzi mkuu ujao, lakini baada ya awamu yake ya pili ni sharti watuunge mkono kama Wapwani ili nasi pia tuingie ikulu.
“Eneo la Pwani limekuwa likimuunga mkono marehemu kinara wetu Bw Raila Odinga na kumpa kura nyingi sana. Hizo kura sasa ni za Ruto. Safari ya kesho inapangwa leo, je, nitafanya makosa kuenda kuomba kura kwa marafiki wa Baba?” aliuliza.
Alimtaka Seneta wa Kericho, Bw Aron Cheruiyot, kupeleka ujumbe kwa Rais Ruto, kuhusu suala hilo la mkataba.
“Tutaunganisha watu wetu waunge mkono Rais Ruto lakini pia mjue kwamba mama zetu wamezaa watu wenye sifa za kuwa rais. Lazima mtuunge mkono baada ya 2027,” alisema Bw Joho.
Kauli ya Joho imeibua mjadala mpya kuhusu mustakabali wa siasa za Pwani, ikionyesha azma ya eneo hilo kutafuta nafasi ya urais mwaka 2032 kupitia makubaliano ya kisiasa na serikali ya sasa.
Bw Joho alisisitiza kuwa Pwani imenufaika kwa kuwa ndani ya serikali na hivyo ni lazima iendelee kushirikiana na Kenya Kwanza.
Hata hivyo, alionya Wapwani dhidi ya kushabikia siasa za upinzani zinazoongozwa na aliyekuwa Naibu Rais, Bw Rigathi Gachagua, na kinara wa chama cha Wiper, Bw Kalonzo Musyoka, akiwataja kama viongozi wanaowahadaa wakazi wa Pwani.
“Walipokuwa serikalini walitusaidia na nini? Mbona leo wanatuita binamu zao? Pia sisi tumejipanga na Rais Ruto. Baada ya Rais Ruto, kiti cha urais kinakuja Pwani. Hatuwafuati bure, tunawafuata kwa mipango. Tuunge Rais tufanye makubaliano ya kulipiana deni. Baada ya Rais kiti kinakuja Pwani,” alisema Bw Joho.
Viongozi wa ODM na UDA walisema wameamua kuweka tofauti zao kando na kushirikiana kumpigia debe Rais Ruto kupata awamu ya pili, wakiahidi kuzuia wapinzani kunyemelea ngome ya ODM.
Naye Gavana wa Mombasa, Bw Abdulswamad Nassir, alisema wanasiasa wa vyama vya ODM na UDA wameamua kuweka tofauti zao za mirengo ya kisiasa kuhakikisha Rais Ruto anarudi mamlakani.
“Huu muungano wa ODM na UDA umeleta maendeleo ambayo mnaendelea kuyaona. Wale walioko upinzani walikuwa wanatubagua walipokuwa mamlakani. Siku hizi wanatuita binamu,” alisema Bw Nassir.
Aliwasihi viongozi wa Pwani kuwa na ushirikiano wa kisiasa unaolenga kuimarisha maendeleo na kuzuia upinzani kunyemelea ngome yao.
Mbunge wa Likoni, Bi Mishi Mboko, alisema Rais Ruto alipata mhamasishaji mkubwa eneo la Pwani baada ya kumteua Bw Joho kwenye baraza lake la mawaziri.
Hivi majuzi, ilibainika Bw Joho anashindania nafasi kubwa ya uongozi katka ODM kupitia kwa wandani wake, hali ambayo huenda ikamlazimu kujiuzulu wadhifa wa uwaziri, huku akiendeleza shinikizo la kuwa mgombea mwenza wa Dkt Ruto katika uchaguzi mkuu ujao.