Kimataifa

Tinubu pazuri kupata Tutam baada ya Upinzani kugawanyika Obi akisisitiza kuwa debeni

Na REUTERS June 3rd, 2026 Kusoma ni dakika: 2

ABUJA, Nigeria:

MWANASIASA wa Nigeria, Peter Obi amesema atagombea tena urais Januari mwakani baada ya kushinda uteuzi wa chama chake, hatua inayozua ushindani mkali dhidi ya rais wa sasa Bola Tinubu pamoja na upinzani uliogawanyika.

Obi alitangazwa mshindi wa kura za mchujo za chama cha Nigeria Democratic Congress, Jumapili, chini ya mwezi mmoja baada ya kujiondoa katika muungano uliokuwa ukijaribu kusimamisha mgombea mmoja wa upinzani.

Kukubali uteuzi huo una maana kuwa Obi ambaye alishika nafasi ya tatu katika uchaguzi uliopita baada ya kuwahamasisha kwa kiasi kikubwa wapiga kura vijana, kunaondoa matumaini ya baadhi ya wafuasi wa upinzani waliokuwa wakitarajia angeweza kurejea katika muungano huo.

Hatua hiyo inaandaa mazingira ya kurudiwa kwa ushindani wa pande tatu ulioshuhudiwa 2023.

Pande hizo zinatarajiwa kupima iwapo hasira za wananchi kutokana na kupanda kwa gharama ya maisha na ukosefu wa usalama zinaweza kutafsiriwa kuwa kura dhidi ya Tinubu, au kama kura za wanaoupinga serikali zitagawanyika tena.

“Lazima tushughulikie ukosefu wa usalama kwa dhamira na haraka, kwa sababu hakuna taifa linaloweza kustawi wakati wananchi wake wanaishi kwa hofu,” akasema Obi.

Nigeria inakabiliwa na migogoro mingi ya kiusalama ambayo ni zaidi ya uasi wa makundi ya jihadi kaskazini mashariki mwa nchi Boko Haram na Islamic State West Africa Province (ISWAP) wamekuwa wakipigana kwa zaidi ya miaka 15 katika eneo hilo.

Kaskazini magharibi, magenge yenye silaha hatari yanayojulikana kama “majambazi” hufanya utekaji wa watu kwa ajili ya fidia pamoja na mashambulizi dhidi ya vijiji na shule.

Wakati huo huo, majimbo ya kaskazini kati pia yamekuwa yakishuhudia mara kwa mara vurugu zinazohusishwa na migogoro ya ardhi na njia za malisho.

Wapiga kura pia wataangazia mageuzi ya kiuchumi ya Tinubu, ikiwemo kuondolewa kwa ruzuku ya mafuta na umeme pamoja na kusitishwa kwa udhibiti wa thamani ya sarafu, hatua ambazo zimevutia wawekezaji hata wakati wananchi wengi wakishuhudia mapato na akiba zao zikidorora.

Kupanda kwa bei ya mafuta duniani kutokana na mzozo wa Iran kumeongeza shinikizo zaidi, huku Nigeria ikishuhudia baadhi ya ongezeko kubwa zaidi la bei ya mafuta miongoni mwa mataifa makubwa ya Afrika.

Ijumaa iliyopita, Tinubu alitetea mageuzi yake ya kiuchumi akisema yameleta utulivu nchini na kurejesha imani ya wawekezaji, licha ya mzigo mkubwa unaowakabili wananchi wa kawaida.

Makamu wa zamani wa Rais, Atiku Abubakar, ambaye alimaliza katika nafasi ya pili katika uchaguzi uliopita, wiki iliyopita alishinda tiketi ya kuwania urais kupitia chama cha African Democratic Congress, katika kile kitakachokuwa jaribio lake la saba kugombea urais.

Viongozi wa vyama vingine vidogo vya kisiasa pia wanatarajiwa kuingia katika kinyang’anyiro hicho.