Habari Mseto

EACC kuandama viongozi wanaobandika majina yao kwenye miradi ya umma

Na ERIC MATARA June 25th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

TUME ya Maadili na Kupambana na Ufisadi (EACC) imewaonya viongozi wanaoweka picha, majina na alama zao za kisiasa kwenye miradi inayofadhiliwa kwa fedha za umma kuwa wanahatarisha kufunguliwa mashtaka na hata kuzuiwa kugombea nyadhifa za uchaguzi siku zijazo.

Onyo hilo linawalenga magavana, wabunge na madiwani ambao wamekuwa wakihusishwa na miradi iliyo na majina, picha au rangi zao za vyama vyao vya kisiasa licha ya miradi hiyo kufadhiliwa na walipa ushuru.

Katika miaka ya hivi majuzi, imekuwa kawaida kuona picha za viongozi kwenye mabango, vibao vya miradi, madarasa, zahanati, barabara, masoko na miradi ya maji iliyojengwa kwa fedha za umma.

Wafuasi wao husema hatua hiyo ni njia ya kuonyesha uwajibikaji, lakini wakosoaji wanaona ni matumizi mabaya ya rasilimali za umma kwa manufaa ya kisiasa.

Afisa Mkuu Mtendaji wa EACC Dkt Abdi Mohamud, alisema tume imepokea ripoti nyingi kuhusu viongozi wanaojitwalia sifa za miradi iliyofadhiliwa na walipa ushuru kwa kuweka majina na picha zao.

“Baadhi ya viongozi wamekuwa wakitumia majina, picha na alama zao kwenye miradi ya umma. Viongozi kama hao wanakabiliwa na hatari ya kushtakiwa na hata kuzuiwa kushiriki uchaguzi,” alisema.

Kwa mujibu wa EACC, Katiba inawataka viongozi kuweka maslahi ya umma mbele ya maslahi binafsi au ya kisiasa na kuhakikisha matumizi ya fedha za umma yanafanywa kwa uwajibikaji.

Tume hiyo imeagiza taasisi za serikali kuhakikisha miradi yote ya umma inatambulishwa kwa jina la taasisi husika pekee na kubainisha iwapo imefadhiliwa na serikali ya kitaifa au ya kaunti bila kuweka picha au majina ya viongozi.

Hatua hiyo pia inaungwa mkono na Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC). Afisa mmoja mkuu wa IEBC alisema tume hiyo inashirikiana na EACC kuhakikisha wanaotaka kugombea nyadhifa mbalimbali wanatimiza masharti ya uadilifu kabla ya kuidhinishwa.

Wakati huo huo, makundi ya kijamii yamezidisha shinikizo kwa Seneti kutunga sheria kali za kuzuia viongozi kupachika majina kwenye miradi ya umma.

Mwanaharakati wa haki za kiraia kutoka Nakuru, Laban Omusundi, amewasilisha ombi katika Seneti akitaka sheria ibadilishwe ili kupiga marufuku magavana na madiwani kutumia picha au majina yao kwenye miradi inayofadhiliwa na walipa ushuru.

Badala yake, amependekeza miradi yote ya umma iwe na maandishi yanayosema: “Kwa Hisani ya Walipa Ushuru wa Kenya.”

“Miradi hii ni mali ya walipa ushuru. Haipaswi kuonekana kana kwamba viongozi wanatumia pesa zao binafsi kuwafanyia wananchi hisani,” alisema.

Mtaalamu wa utawala bora David Ngugi amesema tabia hiyo imekuwepo kwa miaka mingi huku miradi ya serikali ikiendelea kuhusishwa na viongozi walio mamlakani.

Alisema miradi ya maendeleo imegeuzwa jukwaa la kujitangaza kisiasa na kujenga watu binafsi badala ya kuzingatia mchango wa walipa ushuru ambao ndio wanaofadhili maendeleo hayo.