Dimba

DRC na Ghana miongoni mwa mataifa 9 ya Afrika ndani ya raundi ya 32 Kombe la Dunia

Na TOTO AREGE June 28th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

JAMHURI ya Kidemokrasia ya Congo (DRC), na Algeria ni miongoni mwa mataifa tisa kati ya 10 ya Afrika ambayo yamefuzu raundi ya 32 Kombe la Dunia.

DRC walipata ushindi wao wa kwanza kabisa katika Kombe la Dunia baada ya kuichapa Uzbekistan 3-1 na kufuzu hatua ya 32 bora.

Uzbekistan walitangulia kupitia Eldor Shomurodov katika dakika ya 10, lakini DRC waligeuza mchezo kipindi cha pili.

Yoane Wissa alisawazisha kwa mkwaju wa penalti kabla ya Fiston Mayele kufunga bao la pili dakika ya 78. Wissa alikamilisha ushindi kwa bao la tatu muda wa nyongeza.

Ushindi huo uliifanya DRC kumaliza nafasi ya tatu katika Kundi K na sasa watavaana na Uingereza raundi ya 32.

Kwa Uzbekistan, ilikuwa ni kichapo cha tatu mfululizo katika ushiriki wao wa kwanza kabisa wa Kombe la Dunia.

Algeria nao walijihakikishia nafasi katika hatua ya 32 bora baada ya kutoka sare ya 3-3 dhidi ya Austria katika mechi ya kusisimua ya Kundi J.

Nahodha Riyad Mahrez alifunga mabao mawili na kutwaa tuzo ya mchezaji bora wa mechi. Bao lake la pili katika muda wa nyongeza lilionekana kuipa Algeria ushindi, lakini Sasa Kalajdzic aliisawazishia Austria katika dakika ya sita ya muda wa majeruhi.

Matokeo hayo yaliifanya Austria kumaliza ya pili kundini huku Algeria wakifuzu kama mojawapo ya timu bora zilizomaliza nafasi ya tatu.

Mechi hiyo ilikuwa miongoni mwa mechi zilizovutia zaidi katika hatua ya makundi, ikiwa na mabao sita na mabadiliko ya mara kwa mara ya uongozi kabla ya kumalizika kwa sare iliyowapeleka mataifa yote mawili katika hatua ya mwondoano.

Katika mechi zingine, Croatia walifuzu hatua ya 32 bora baada ya kuibuka na ushindi wa 2-1 dhidi ya Ghana katika mechi ya mwisho ya Kundi L iliyochezwa Philadelphia.

Petar Sucic aliwapa Croatia uongozi katika dakika ya 31 kwa shuti kali la mbali kabla ya Derrick Luckassen kuisawazishia Ghana dakika ya 73.

Nikola Vlasic aliifungia Croatia bao la ushindi dakika ya 83 kwa kichwa, na kuwainua hadi nafasi ya pili kundini.

Hii ni mara ya kwanza kwa Black Stars kutinga hatua ya hii tangu Kombe la Dunia la 2010 nchini Afrika Kusini, walipokaribia kufuzu nusu fainali kabla ya kutolewa na Uruguay kwa mikwaju ya penalti.

Katika mechi zingine,  Jordan walipata ushindi wa 3-1 dhidi ya mabingwa watetezi Argentina nao Uingereza wakainyorosha Panama 2-0.