Unganisheni Wakenya badala ya kujitokeza tu wakati wa uchaguzi, Wetang’ula ahimiza NCIC
Spika wa Bunge la Kitaifa, Moses Wetang’ula, amehimiza Tume ya Uwiano na Utangamano wa Kitaifa (NCIC) kurejesha imani ya Wakenya na kuwa mstari wa mbele kuimarisha umoja wa taifa wakati wote, badala ya kujitokeza tu kipindi cha uchaguzi.
Wetang’ula alisema tume hiyo ilianzishwa baada ya ghasia za baada ya uchaguzi wa mwaka 2007 ili kuponya migawanyiko ya kisiasa, lakini imeendelea kukumbwa na changamoto ya kutokuaminiwa na wananchi.
“NCIC ina tatizo kubwa la kuaminiwa. Haipaswi kuonekana kama taasisi inayofanya kazi wakati wa uchaguzi pekee,” alisema alipokutana na viongozi wa tume hiyo wakiongozwa na mwenyekiti wake, Askofu Kepha Omae, katika majengo ya Bunge.
Alisisitiza kuwa elimu endelevu kwa wananchi ndiyo njia bora ya kubadili mitazamo na kujenga mshikamano wa kudumu.
“Hakuna tatizo mtu kuwa wa jamii fulani. Tatizo ni pale utambulisho huo unapotumiwa kuwabagua au kuwanyanyasa wengine,” alisema.
Wetang’ula pia aliitaka NCIC kushirikiana kwa karibu na Wizara ya Elimu ili kukuza utamaduni wa umoja miongoni mwa wanafunzi na vijana.
Aidha, alihimiza tume hiyo kuimarisha ushirikiano na Idara ya Upelelezi wa Jinai (DCI), Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka ya Umma (ODPP), Mahakama na Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) ili kuongeza ufanisi wake.
“Mnayo mamlaka ya kuchunguza, lakini mashtaka yanaendeshwa na DPP. NCIC inapaswa kujijengea heshima kwa kufanya kazi kwa weledi. Bunge litaendelea kuunga mkono kwa mujibu wa sheria,” alisema.
Spika huyo aliongeza kuwa uchaguzi ni mchakato unaoendelea na si tukio la siku moja, hivyo NCIC ina jukumu muhimu la kukabiliana na matamshi ya chuki na viongozi wanaochochea migawanyiko.
Kwa upande wake, Askofu Kepha Omae alisema tume tayari imeanza maandalizi ya Uchaguzi Mkuu wa 2027 kupitia mpango unaolenga kuzuia migogoro, kuimarisha ushirikiano na kushirikisha wadau mbalimbali.
“Tumeandaa ramani ya utekelezaji. Tunataka kushirikiana na taasisi nyingine na viongozi wa kisiasa ili kupunguza ubaguzi na ukabila,” alisema.
Aliongeza kuwa NCIC itafanya kazi kwa karibu na wazee wa jamii, viongozi wa dini, shule na taasisi nyingine za elimu ili kuhamasisha siasa za amani na kuwataka viongozi kupunguza matamshi ya uchochezi.
Kamishna wa NCIC Jerusha Mwaathime alitaka Bunge kupatia tume mamlaka makubwa zaidi ya uchunguzi ili iweze kushughulikia kwa ufanisi visa vinavyochochea chuki na migawanyiko nchini.