Tofauti zaibuka kuhusu tarehe ya kuandaa uchaguzi
INGAWA Katiba ya 2010 iliweka tarehe ya uchaguzi ili iwe wazi na ya kutabirika, suala hilo limefikishwa mahakamani angalau mara tano tangu 2015.
Kesi hizo zimehusisha majaji 13 na kuzua tafsiri tofauti kuhusu maana ya kifungu kinachosema uchaguzi ufanyike “Jumanne ya pili ya Agosti katika kila mwaka wa tano”.
Mzozo huo umeibuka tena baada ya Jaji wa Mahakama Kuu Malindi Mugure Thande kuamua kuwa uchaguzi mkuu ulipaswa kufanyika Agosti 2026 badala ya 2027.
Mwanasheria wa masuala ya Katiba Waikwa Wanyoike anasema mkanganyiko huo unatokana na dhana kwamba Katiba inamhakikishia kila kiongozi aliyechaguliwa kipindi cha miaka mitano.
Vita vya kwanza vilianza kabla ya uchaguzi wa 2017 baada ya watu watatu kupinga tarehe iliyokuwa imewekwa na Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka nchini (IEBC).
Walidai kuwa uchaguzi wa madiwani wa kaunti (MCAs) Agosti 8, 2017 ungekatiza kipindi chao cha miaka mitano kwa karibu miezi minane.
Jaji Edward Muriithi aliamua Aprili 2017 kuwa kulikuwa na mkanganyiko kati ya vifungu viwili vya Katiba kuhusu muda wa madiwani na tarehe ya uchaguzi.
Hata hivyo, Mahakama ya Rufaa ilibatilisha uamuzi huo Novemba 2017 na kusema tarehe ya uchaguzi iliyowekwa na Katiba haiwezi kubadilishwa.
Kesi nyingine iliwasilishwa mwaka 2018 na mwanaharakati Okiya Omtatah na Nyakina Wycliffe Gisebe. Walidai uchaguzi ulipaswa kufanyika Agosti 2021 badala ya 2022.
Jaji Weldon Korir alikataa kesi hiyo Novemba 2020, akisema uchaguzi wa viongozi wote unapaswa kufanyika siku moja baada ya kipindi cha miaka mitano.
Mwaka 2022, aliyekuwa Seneta mteule Paul Njoroge alipinga tarehe ya uchaguzi wa urais wa Agosti 9. Jaji Anthony Mrima alikataa hoja hiyo.
Mzozo huo ulifika Mahakama ya Juu mwaka 2025 baada ya mwanasheria Dkt Owiso Owiso na wanaharakati Khelef Khalifa na Ashioya Biko kutaka mahakama hiyo ieleze kifungu cha 136(2)(a).
Mahakama hiyo ya majaji saba haikugusia kiini cha kesi na ikaiondoa Agosti 15, 2025 kwa misingi ya mamlaka yake.
Walalamishi hao walienda Mahakama Kuu ya Malindi, ambako Jaji Thande aliamua kuwa uchaguzi mkuu ulipaswa kufanyika Jumanne, Agosti 11, 2026.
Bw Wanyoike anaunga mkono tafsiri hiyo akisema Katiba haimhakikishii Rais, wabunge na maseneta kipindi kamili cha miaka mitano.
Hata hivyo, mwanasheria Dudley Ochiel anapinga akisema historia ya kutunga Katiba inaonyesha wazi kuwa Kenya ilikusudia kuwa na mzunguko wa uchaguzi wa miaka mitano.
“Historia ya Katiba haiungi mkono nia ya kuanzisha vipindi vya miaka minne kwa viongozi waliochaguliwa,” alisema.
Mwanasheria Ndung’u Wangenye anasema Mahakama ya Juu ndiyo itakayotoa jibu la mwisho kuhusu suala hilo.
“Suluhisho la mwisho litakuwa uamuzi wa Mahakama ya Juu,” alisema.