DimbaUncategorized

Kocha wa Harambee Starlets Beldine Odemba aweka imani kwa chipukizi

Na TOTO AREGE June 7th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

LICHA ya timu ya taifa ya soka ya wanawake Harambee Starlets kupoteza 4-1 kwa mikwaju ya penalti dhidi ya Zambia baada ya sare ya 1-1 muda wa kawaida, kocha mkuu Beldine Odemba aliridhishwa na kiwango kilichoonyeshwa na wachezaji chipukizi walioko kikosini.

Mchuano huo wa kupimana nguvu wa mataifa manne ulipigwa Jumamosi katika Uwanja wa Levy Mwanawasa mjini Ndola, Zambia.

Mapema siku hiyo katika uwanja huo, Zimbabwe iliinyorosha Lesotho 3-1 na kufuzu fainali dhidi ya wenyeji Zambia. Kenya sasa itavaana na Lesotho katika mechi ya kutafuta mshindi wa tatu kesho katika uwanja huo.

“Kwa siku nyingi, nimeamini wachezaji chipukizi wanawaweza wakafanya vizuri katika timu ya taifa ndiyo maana unaona wakipewa nafasi,” alisema Odemba baada ya mechi hiyo.

Zambia ilianza kwa kasi na kufunga bao la mapema dakika ya tatu kupitia mshambuliaji Prisca Chilufya kabla ya Starlets kusawazisha kupitia fowadi Fasila Adhiambo dakika ya 77 baada ya kupokea pasi kutoka kwa nguvu mpya Marion Serenge.

Serenge pamoja na beki Elizabeth Ochaka waliocheza dhidi ya Zambia,  walipandishwa kutoka timu ya vijana za Junior Starlets (chini ya miaka 17) na Rising Starlets (chini ya miaka 20), na walikuwa sehemu ya kikosi cha Kenya kilichoshiriki Kombe la Dunia la Wanawake Chini ya Miaka 17 mwaka 2024 nchini Jamhuri ya Dominican.

Beki Lorine Ilavonga na mshambuliaji Lorna Faith, ambao pia walikuwa katika kikosi hicho cha Kombe la Dunia, walisalia benchi mechi yote.

“Tuna wachezaji kutoka timu za chini ya miaka 17 na 20 jambo ambalo linatupa matumaini kwamba, watachukua nafasi ya wachezaji wazoefu watakapoondoka,” aliongezea Odemba.

Kenya, na Zambia zinatumia mashindano hayo kama sehemu ya maandalizi ya Kombe la Mataifa ya Afrika kwa Wanawake (WAFCON) 2026 litakaloandaliwa Morocco kuanzia Julai 25 hadi Agosti 16. Lesotho (177) na Zimbabwe (127) hazikufuzu kwa mashindano hayo.

Odemba alisema ameona maendeleo makubwa katika kikosi chake licha ya maeneo kadhaa yanayohitaji kuboreshwa kuelekea WAFCON.

Kocha wa Zambia Nora Häuptle, alisema kiwango kilichoonyeshwa na Kenya kinaonyesha jinsi soka ya wanawake Afrika inavyoendelea kupiga hatua.

“Soka ya Afrika inakua. Zamani tulikuwa na timu chache zilizokuwa zikitawala mchezo wa wanawake, lakini sasa mambo yanabadilika. Kenya inapiga hatua kubwa, vivyo hivyo Malawi, na ninaamini WAFCON ya mwaka huu itakuwa na ushindani mkubwa,” alisema Häuptle.