Dimba

Morocco yaiondoa Canada, yatinga robo fainali dhidi ya Ufaransa

Na TOTO AREGE July 5th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MOROCCO ilikuwa timu ya kwanza ya Afrika kutinga robo fainali ya Kombe la Dunia la mwaka huu, baada ya kuwanyorosha wenyeji Canada 3-0 na kuhitimisha safari ya taifa hilo kwenye mashindano hayo.

Canada ilianza mechi kwa kasi na kutengeneza nafasi kadhaa za mapema kupitia Jonathan David na Tani Oluwaseyi, lakini mlinda lango Yassine Bono aliokoa juhudi zao na kuwanyima bao.

Morocco ilifungua ukurasa wa mabao dakika ya 50 kupitia Azzedine Ounahi, aliyemalizia pasi kutoka kwa Achraf Hakimi kufuatia mpira wa adhabu.

Ounahi aliifungia Morocco bao la pili dakika ya 82 baada ya shambulizi la kushtukiza kabla ya Soufiane Rahimi kufunga bao la tatu katika muda wa majeruhi na kuthibitisha ushindi wa Simba wa Atlas.

Licha ya Canada kutawala kwa muda mrefu na kugusa mpira mara 30 ndani ya eneo la hatari la Morocco, ilifanikiwa kupiga mashuti matatu pekee yaliyolenga lango huku safu ya ulinzi ya Morocco ikiendelea kung’ara.

Kocha wa Canada Jesse Marsch aliwasifu wachezaji wake licha ya kipigo.

“Kulikuwa na timu moja tu uwanjani mwanzoni mwa mchezo. Tulikuwa bora kuliko timu iliyoorodheshwa nafasi ya saba duniani leo, lakini hatukuweza kutumia nafasi tulizopata,” alisema Marsch.

Hata hivyo, Canada imeondoka ikiwa imeandika historia kwa kufuzu hatua ya mtoano kwa mara ya kwanza na pia kushinda mechi ya kwanza ya hatua hiyo kwenye Kombe la Dunia.

Morocco sasa imeifunga Canada mara mbili mfululizo katika Kombe la Dunia baada ya ushindi wao wa hatua ya makundi mwaka 2022 na haijapoteza katika mikutano mitano dhidi ya taifa hilo.

Ufaransa yaivuka Paraguay kwa tabu, yakutana na Morocco robo fainali

Penalti ya kipindi cha pili ya nyota Kylian Mbappe, iliipa Ufaransa ushindi mwembamba wa 1-0 dhidi ya Paraguay na kuipeleka robo fainali ya Kombe la Dunia 2026.

Paraguay ilijipanga vyema na kuzuia mashambulizi ya Ufaransa kwa kipindi kizima cha kwanza huku hakuna timu iliyopiga shuti lililolenga lango.

Mchezo uliamuliwa dakika ya 72 baada ya Desire Doue kuangushwa ndani ya eneo la hatari na Diego Gomez. Baada ya ukaguzi kwa VAR, mwamuzi Ilgiz Tantashev aliamuru penalti ipigwe.

Mbappe hakukosea kutoka hatua ya penalti na kumshinda kipa Orlando Gill, akifunga bao lililowapeleka Les Bleus hatua ya robo fainali.

Bao hilo limemfikisha Mbappe mabao saba kwenye mashindano haya, sawa na Lionel Messi katika mbio za kuwania Kiatu cha Dhahabu.

Paraguay, waliowashangaza wengi kwa kuwaondoa Ujerumani kwa mikwaju ya penalti katika hatua ya 32 bora, waliwapa wakati mgumu mabingwa hao wa 2018 kwa ulinzi madhubuti na mchezo wa nguvu.

Hata hivyo, kasi ya Doue baada ya kuingia kipindi cha pili ilibadilisha kasi ya mchezo na kumpatia Mbappe nafasi ya kuamua matokeo.

Ufaransa sasa itakutana na Morocco katika robo fainali itakayochezwa Boston Julai 9, huku Paraguay ikimaliza safari yake ya Kombe la Dunia 2026.