Kimataifa

Idadi ya walioangamia nchini Nepal yafika 470

Na MASHIRIKA, WINNIE ONYANDO August 29th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

WITO umetolewa kwa mataifa mbalimbali kuingilia kati ili kuisaidia nchi ya Nepal baada ya idadi ya waliofariki kutokana na mafuriko makubwa yaliyokumba maeneo ya milimani ikiwa zaidi ya 470 huku zaidi ya watu 1,000 wakiendelea kutafutwa.

Waokoaji wanaendelea kukagua mabonde na vijiji vilivyofunikwa na matope, mawe na vifusi baada ya mafuriko makubwa yaliyotokea Jumatano.

Janga hilo lilitokea baada ya sehemu ya barafu katika Milima ya Himalaya kuyeyuka na kusababisha mkondo mkubwa wa maji, matope na mawe kuingia kwenye mito ya milimani.

Awali kulikuwa na dhana kwamba tetemeko la ardhi ndilo lililosababisha maafa hayo, lakini uchunguzi wa baadaye ulionyesha kuwa kuyeyuka kwa barafu na miamba ndiko kulikosababisha mafuriko hayo.

Mafuriko hayo yameathiri vibaya eneo la Rasuwa na maeneo mengine kaskazini mwa Nepal, karibu na mpaka wa China.

Vijiji, barabara, madaraja na miundombinu mingine vimeharibiwa, hali inayofanya shughuli za uokoaji kuwa ngumu.

Taarifa za mamlaka ya utalii Nepal zinaonyesha kuwa watalii 667 hawajulikani waliko, wakiwemo raia wa nchi 31.

Takribani wageni 540 kati yao ni raia wa kigeni. India imeorodhesha raia wake 288 waliopotea, huku Amerika ikiwa na angalau 65, Malaysia 55, Ukraine 53, Uingereza 33, Australia 25 na Canada 25.

Mafuriko pia yameathiri upande wa Tibet unaodhibitiwa na China.

Katika jimbo la Gyirong, watu 558, wakiwemo raia 260 wa kigeni, wameripotiwa kupotea, huku China ikithibitisha vifo vitatu.

Serikali za Nepal na China zimepeleka helikopta na vikosi vya uokoaji katika maeneo yaliyoathirika.

Hata hivyo, barabara zilizokatika na mawasiliano kuvurugika vimeathiri juhudi za kuwafikia manusura.

Wakati huo huo, mamlaka zimeonya kuhusu hatari nyingine ya mafuriko baada ya maji kuziba sehemu ya Mto Bhotekoshi na kuunda ziwa linaloweza kuvunja kingo na kusababisha mafuriko zaidi.

Wakazi katika maeneo yaliyo hatarini wameonywa kuwa tayari kwa uokoaji.

Nepal hupokea mvua nyingi wakati wa msimu wa monsoon, lakini wataalamu wameonya kuwa mabadiliko ya hali ya hewa yanaongeza hatari ya kuyeyuka kwa barafu na kutokea kwa mafuriko makubwa.

Shughuli za uokoaji zinaendelea huku familia zikisubiri taarifa kuhusu ndugu zao waliopotea.