• Nairobi
  • Last Updated April 20th, 2024 5:55 AM
2022: ‘Kieleweke’ wamrai Ruto amteue Muturi mgombea mwenza

2022: ‘Kieleweke’ wamrai Ruto amteue Muturi mgombea mwenza

NA DANIEL OGETTA

KUNDI la wabunge wa ‘Kieleweke’ kutoka Mlima Kenya sasa wanamtaka Naibu Rais, Dkt William Ruto kumteua Spika wa Bunge Justin muturi kama mwaniaji mwenza katika kinyang’anyiro cha urais hapo 2022.

Wakiongozwa na mbunge wa Mbeere Kaskazini Muriuki Njagagua, walisema watafurahia iwapo Naibu Rais atamteua Bw Muturi kama mwenza wake katika kinyang’anyiro hicho.

Wabunge hao wanasema kwamba Bw Muturi hajahusika kwa namna yoyote katika ufisadi wala unyakuzi wa mali ya umma na kwamba anayo tajriba katika kutumikia umma.

Hata hivyo, mnamo 1997, Bw Muturi alituhumiwa kula rushwa alipokuwa hakimu, lakini Tume ya Huduma ya Mahakama (JSC) ikafuta madai hayo.

Wabunge hawa walikuwa wakizungumza katika hafla ya kumpongeza mbunge wa Manyatta Bw John Muchiri. Bw Njagagua alisema kwamba Bw Muturi anamfaa Bw Ruto ambaye alihudhuria hafla hiyo, kama mwaniaji mwenza.

Bw Njagagua aliungwa mkono na Mbunge wa Kikuyu, Bw Kimani Ichungw’a aliyesema wakazi wa Embu wamekuwa wakiunga mkono serikali zilizopita hivyo basi hawafai kusahaulika katika uteuzi wa kujaza nafasi kubwa serikalini.

“Wakazi wa Embu walimuunga mkono Mzee Jomo Kenyatta, Daniel Moi na Mwai Kibaki na hata kuipigia serikali ya Jubilee kura. Hivyo basi kile ambacho wakazi hawa wa Embu wataamua ndicho kitafanyika,” alisema Ichungw’a.

Mbunge wa Tharaka Nithi, Bw Murugara Gitonga naye akasema atazungumza na Spika wa Seneti Bw Kithure Kindiki ambaye pia anamezea mate kuwa mgombea mwenza ili amruhusu Bw Muturi kuchukua nafasi hiyo.

Mbunge maalum Bi Cecile Mbarire naye alisema kwamba 2022 utakuwa wakati mwafaka wa wakazi wa Mlima Kenya kumshukuru Bw Ruto kwa kumuunga mkono rais Kenyatta. Akizungumzia pendekezo hilo, Naibu wa Rais alisema kwamba wakati ukiwadia, chama cha Jubilee ndiyo itaamua atakayenyakua wadhfa huo.

Akielezea kukubaliana na maoni ya wabunge hawa, Dkt Ruto alisema kwamba Bw Muturi ana ujuzi ufaao kwani alipokuwa kwenye upinzani, Bw Muturi alikuwa kiongozi katika chama. Dkt Ruto pia aliwarai wakazi wa Embu kuzidi kuunga mkono utendakazi wa serikali ya Jubilee kwa muda uliosalia.

Bw Muturi anyejulikana kwa jina la utani kama ‘JB’, alikuwa mbunge wa kwanza wa Siakago kuchaguliwa katika uchaguzi mdogo wa 1997 kwa tiketi ya KANU alipoaga Silas Ita.

Wabunge wengine waliohudhuria hafla hiyo ni Alice Wahome (Kandara), Geoffrey King’ang’i (Mbeere South), Erick Muchangi (Runyenjes), Gichohi Mwangi na Njeru Ndwiga (Seneta wa Embu).

You can share this post!

Chifu kizimbani kwa kuiba mbwa!

Karoney akiri serikali ilitoa hati miliki zenye kasoro

adminleo