Habari Mseto

Bei ghali ya mafuta kupandisha gharama ya maisha

February 20th, 2018 1 min read

Kituo cha mafuta cha National Oil. Bei ya mafuta imekuwa ikipanda kwa miezi sita mfululizo tangu Septemba 2017. Picha/ Maktaba

Na BERNARDINE MUTANU

BEI ya mafuta inazidi kupanda nchini, na wananchi wanafaa kutarajia ongezeko la gharama ya maisha.

Kwa miezi sita mfululizo tangu Septemba 2017, bei ya mafuta imeonekana kupanda ambapo katika jendwali jipya la bei ya petroli ilipanda kwa Sh1.62 na Sh2.14 kwa dizeli, ilhali bei hiyo kwa mafuta taa ilipanda kwa Sh1.97.

Kulingana na shirika la kutetea haki za wateja (Cofek) huenda kupanda kwa bei ya mafuta kukasababisha kupanda kwa nauli ya magari.

Cofek ilisema huenda kukawa na ongezeko la matumizi ya mafuta chafu, hali inayotarajiwa kuathiri zaidi afya na magari.

Makampuni mengi hutumia mafuta katika kutengeneza bidhaa, huenda hali hiyo ikaathiri gharama ya uzalishaji wa bidhaa, alisema Mkurugenzi wa Chama cha Watengenezaji Bidhaa (KAM) Bi Phyllis Wakiaga.

Kulingana na ripoti ya Benki ya Dunia, bei za mafuta zitazidi kuongezeka hadi Sh5, 796 kwa pipa, kutoka Sh5, 485.5.

Wauzaji wa mafuta katika soko la kimataifa wamekubaliana kupunguza kiwango cha uzalishaji wa mafuta ili kudhibiti bei katika soko la kimataifa.

Uamuzi huo unaathiri bei ya mafuta moja kwa moja, hali itakayowazidishia mzigo wa gharama ya maisha wananchi.