• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 1:15 PM
Siwezi kujaza fomu za uraia, afoka Miguna Miguna

Siwezi kujaza fomu za uraia, afoka Miguna Miguna

Na STELLA CHERONO na BENSON MATHEKA

WAKILI mbishi Dkt Miguna Miguna anaendelea kuzuiliwa katika uwanja wa Kimataifa wa Ndege wa  Jomo Kenyatta (JKIA) Nairobi huku wakili wake  Cliff Ombeta akisema hatajaza fomu alizopatiwa na idara ya uhamiaji.

Bw Ombetta alisema Jumanne kwamba mteja wake hataomba upya uraia wa Kenya kwa sababu kufanya hivyo ni sawa na Miguna kukubaliana na serikali kwamba hakuwa raia wa Kenya.

Aliitaka serikali kuheshimu agizo la Mahakama Kuu ambalo iliagiza Miguna kurudi Kenya baada ya kupelekwa Canada kinyume cha sheria.

“Anapaswa kuruhusiwa kuingia Kenya kwa nguvu za agizo la mahakama,” Bw Ombetta aliambia wanahabari katika uwanja wa ndege wa Jomo Kenyatta (JKIA).

Alisema kujaza fomu alivyotakiwa na idara ya uhamiaji ni kumaanisha kwamba Miguna anakubali kwamba serikali ilikuwa sawa tangu mwanzo kwamba alikuwa nchini kinyume cha sheria.

“Serikali inataka atumie paspoti yake ya Canada kuthibitisha vitendo vyake, wanataka apatiwe viza ili iweze kumpimia muda atakaokuwa Kenya,” alisema.

Alisema kwamba Mahakama Kuu iliagiza serikali ihakikishe wakili huyo amerudi Kenya na kumpatia paspoti na sio kuomba mpya.

“Mahakama ilisema anafaa kuwa nchini hadi kesi yake imalizike. Hatujui itachukua muda gani. Mahakama iliagiza aruhusiwe kuingia Kenya bila masharti,” alisema Bw Ombetta.

Bw Ombetta ambaye aliandamana na katibu mkuu wa  ODM  Edwin Sifuna,  hakuruhusiwa kuingia eneo ambalo Miguna amefungiwa katika chumba kimoja. Alisema haruhusiwi kuona yeyote.

Kufikia adhuhuri Jumanne, mawakili  James Orengo na Otiende Amollo  walikuwa katika eneo la kusubiri wageni wakitarajia kumuona na kuzungumza na Bw Miguna.

Maafisa wa kikosi cha kupambana na fujo (GSU) waliwafukuza mawakili na wanahabari na kuzingira eneo ambalo Miguna amezuiwa.

You can share this post!

Fisi afunzwa adabu kwa kutamani visivyolika

Raila aapa kushtaki Facebook na Cambridge Analytica kwa...

adminleo