• Nairobi
  • Last Updated April 23rd, 2024 9:40 PM
Ruto awapa onyo wabunge wa Jubilee

Ruto awapa onyo wabunge wa Jubilee

Naibu Rais William Ruto. Picha/ Maktaba

Na VALENTINE OBARA

NAIBU Rais, Bw William Ruto, ameonya wabunge wa Jubilee dhidi ya kuzusha fujo zinazoweza kusababisha mgawanyiko wa wananchi.

Akizungumza Jumapili katika eneo la Mwea, Kaunti ya Kirinyaga, Bw Ruto alisema mienendo hiyo itafanya iwe vigumu kwa Rais Uhuru Kenyatta kutekeleza ajenda zake za maendeleo kabla kukamilisha hatamu yake ya uongozi.

“Kuna watu wana ushujaa wa kelele ya fujo na fitina lakini sisi katika Jubilee tunajua siasa zetu ni za kuunganisha Wakenya na kuleta maendeleo. Nawaomba viongozi wote hasa wa Jubilee, tujitahidi kutimiza manifesto yetu,” akasema.

Ingawa hakutaja wanasiasa wowote, matamshi yake yalitokea wakati ambapo kuna mvutano kati ya Gavana wa Kaunti ya Kirinyaga, Bi Anne Waiguru, na Mbunge Mwakilishi wa kaunti hiyo, Bi Wangui Ngirici, kufuatia kisa ambapo fujo zilizuka kwenye mkutano wa hadhara wa Bi Waiguru wiki iliyopita.

Katika ziara yake, naibu wa rais alitangaza mipango ya serikali kuimarisha miradi mbalimbali katika kaunti hiyo ikiwemo ya barabara, afya, uzalishaji wa chakula cha kutosha na usambazaji wa maji.

“Nawaomba viongozi wote hasa wa Jubilee, tulikubaliana kwamba mambo yetu ni mawili: Kuunganisha Kenya yote na kuondoa siasa ya mgawanyiko, na pili ni maendeleo. Nataka niwaombe nyinyi nyote muungane, tushirikiane ili tuunganishe Wakenya wote na tuharakishe maendeleo yetu ya Kenya,” akasema.

You can share this post!

Waboni waitaka serikali iwajengee shule ya bweni

Ingwe yaponea kichapo

adminleo