• Nairobi
  • Last Updated April 20th, 2024 6:55 AM
Wakazi wa Mokowe kunufaika na mradi wa ujenzi wa vyoo

Wakazi wa Mokowe kunufaika na mradi wa ujenzi wa vyoo

Na KALUME KAZUNGU

ZAIDI ya wakazi 5,000 wa mji wa Mokowe, Kaunti ya Lamu watanufaika na mradi uliozinduliwa wa Sh17.2 milioni wa ujenzi wa vyoo 200 na uimarishaji wa mabomba ya majitaka eneo hilo.

Mradi huo unaofadhiliwa na serikali ya Kenya chini ya Bodi ya Hazina ya Maji kwa ushirikiano na wakfu wa Bill na Melinda Gates unalenga hasa kuimarisha usafi miongoni mwa wakazi wa kipato cha chini wanaoishi mijini hasa kupitia kuboreshwa kwa miundomsingi ya kumwaga majitaka.

Akizungumza wakati wa uzinduzi wa mradi huo katika ofisi za Shirika la Kusambaza Maji kwa wakazi wa Lamu (Lawasco), Afisa wa Miradi na Mipango wa Bodi ya Hazina ya Maji (Water Sector Trust Fund), Bi Fresiah Muiyuro alisema lengo la shirika lake ni kuhakikisha wanaboresha miundomsingi, hasa vyoo na mabomba ya kupitisha maji taka kwenye kaunti zote 20 ambako mradi huo unatekelezwa.

“Tulipokea maombi 42 kutoka kaunti mbalimbali za hapa nchini zilizotaka fedha za kujenga vyoo na kuimarisha hali ya mabomba ya kupitisha maji taka. Ni kaunti 20 pekee, ikiwemo Lamu ambazo zilipasishwa kupata mgao huo. Hii ndiyo sababu tuko hapa leo kukabidhi LAWASCO hundi ya Sh 17.2 milioni za kutekelezea mradi huo kwenye mji unaolengwa wa Mokowe. Fedha hizo zitatekeleza ujenzi wa vyoo 200 kwa wakazi mjini humo na pia kuimarisha hali ya utupaji wa maji-taka,” akasema Bi Muiyuro.

Gavana wa Lamu, Fahim Twaha ambaye alikuwepo wakati wa shughuli ya kukabidhi LAWASCO hundi hiyo aliishukuru serikali ya Kenya, Bodi ya Hazina ya Maji na pia wakfu wa Bill and Melinda Gates kwa kuhakikisha Lamu inajumuishwa kwenye mpango huo.

Bw Twaha alisema serikali yake imekuwa ikikumbwa na changamoto tele hasa katika kuimarisha mambomba ya maji taka eneo hilo kutokana na kwamba mpangilio ulioko ni wa zamani na ni vigumu kuubadilisha.

Alitaja mradi wa ujenzi wa vyoo 200 na pia kuimarishwa kwa mambomba ya kumwaga maji taka mjini Mokowe kujiri kwa wakati ufaao.

“Kama kaunti tulikuwa mbioni kujaribu kukarabati na kuimarisha hali ya usafi wa miji yetu, ikiwemo jinsi maji-taka yanavyotupwa. Tunashukuru kwamba serikali ya kitaifa, Hazina ya Bodi ya Maji nchini na wakfu wa Bill and Melinda Gates wametukumbuka na kutoa fedha za kuboreshea vyoo mjini Mokowe. Tutaendelea kushirikiana kwa suala hilo hadi mwisho,” akasema Bw Twaha.

Mkurugenzi wa Bodi ya Kusambaza Maji Lamu (Lawasco), Paul Wainaina, alisema mradi wa ujenzi wa vyoo na kuimarishwa kwa miundomsingi ya umwagaji maji-taka mjini Mokowe itatekelezwa na kukamilika katika kipindi cha miezi mitatu au minne ijayo.

Bw Wainaina aliwarai maafisa wa Bodi ya Hazina ya Maji nchini kuongezea kaunti ya Lamu mgao zaidi ili kuendeleza uboreshaji wa vyoo na miundomsingi ya utupaji maji-taka kwenye miji mbalimbali ya eneo hilo, ikiwemo Hindi, Witu, Kiunga na sehemu zingine.

“Baada ya kupokea hundi ya Sh 17.2 milioni kutoka kwa bodi ya hazina ya maji, tayari tumeanza kukabishi wenye nyumba kati ya Sh15,000 hadi Sh20,000 kwa kila choo ili kuviboresha. Nikon a hakika kwamba shughuli hiyo itakamilika kati ya miezi mitatu au minne. Ombi langu kwa bodi ya hazina ya maji ni kwamba iongezee Lamu mgao zaidi ili kuendeleza miradi kwenye sehemu zingine za kaunti,” akasema Bw Wainaina.

Afisa Msimamizi wa Bodi ya Hazina ya Maji, tawi la Lamu, Hussein Kuso alisema mbali na kuboresha hali ya afya kwa wakazi, mradi huo pia unalenga kutibu kinyesi kutoka kwa vyoo husika, ambapo mabaki yatatumika kama mbolea kwa wakulima.

You can share this post!

KINA CHA FIKIRA: Waswahili wameonyesha utu kumuenzi Maulidi...

SEKTA YA ELIMU: Magoha atoe mipango thabiti ya mageuzi...

adminleo