• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 7:00 PM
FUNGUKA: Nachuuza mke wangu nipate hela

FUNGUKA: Nachuuza mke wangu nipate hela

 

Na PAULINE ONGAJI

Japo mwanzoni nilionekana kukerwa na tabia hii, mke wangu alinishawishi akisema kwamba ingekuwa fursa murwa ya kuangamiza ufukara uliotukodolea macho kwa kumwalika mwanamume huyo kwenye meza yetu na kumhadaa kuwa mimi ni dadake – Vitalis

Kuna dhana kuwa kati ya jinsia mbili zinazotambulika, hakuna watu waliojawa na wivu kama wanaume.

Hii ni hasa inapowadia katika masuala ya mahaba ambapo ni dhahiri kuwa wanaume hupata maumivu makali mwanamke wampendaye anapoamua kugawa asali pembezoni.

Kwa mfano ni rahisi kwa mwanamke kumsamehe mwanamume anapomlaghai katika uhusiano, lakini huwia vigumu wanaume kufanya hivyo.
Hili linadhihirishwa kila tunaposikia visa vya wanaume kuwaua wapenzi wao kwa sababu ya udanganyifu katika uhusiano.

Lakini kwa Vitalis mambo ni tofauti sana. Huku wanaume wengi wakiwakinga wapenzi, wachumba na wake zao kutokana na macho ya madume wenye tamaa, bwana huyu anafanya kila awezalo kuwavutia madume wenzake kwa mkewe Rita.

Wawili hawa wameoana kwa miaka minne na wana watoto wawili lakini penzi lao ni la kushangaza ajabu. Kwanza kabisa hawana ajira na wamekuwa wakitegemea fedha kutoka kwa wanaume wengine kukidhi mahitaji yao ya kila siku.

Vitalis amekuwa akimchuuza mkewe kwa wanaume hasa wa kizungu huku wawili hawa wakijifanya kuwa mandugu kila wanapokutana na windo lao.
Kulingana na Vitalis tabia hii ilianza miezi michache baada ya kuoana.

“Nilikuwa nimefanya kibarua na kupata senti kidogo ambapo niliamua kumpeleka mke wangu angaa katika mkahawa wa kifahari ili kupata kikombe cha kahawa.

Kutokana na umbo lake la kupendeza na urembo wake wa kipekee alivutia macho ya wengi mle ndani. Hasa alinasa macho ya bwana mmoja wa kizungu ambaye alikuwa akimkodolea macho bila haya.

Japo mwanzoni nilionekana kukerwa na tabia hii, mke wangu alinishawishi akisema kwamba ingekuwa fursa murwa ya kuangamiza ufukara uliotukodolea macho kwa kumwalika mwanamume huyo kwenye meza yetu na kumhadaa kuwa mimi ni dadake.

Kwa hivyo tulimualika na hata kuagiza vinywaji kwa pamoja. Baadaye ilikuwa kawaida kwa dume hilo kututembelea nyumbani kwetu ambapo alimchumbia mke wangu kwa miaka miwili tukiwa pamoja.

Mojawapo ya maagano kati ya yake na mke wangu ilikuwa kununua nyumba na kuwekeza hapa Kenya. Kutokana na kuwa kaka huyo alikuwa ameduwazwa na penzi la mke wangu, katika kipindi cha miezi sita alikuwa ashatimiza haya lakini pindi alipoanza kusisitiza amzalie mtoto, binti akachana mbuga na kutoweka na mali yote.

Tokea tuanze biashara hii tumehadaa wanaume watano wa kizungu na hata kuna wengine ambao wanazidi kukidhi mahitaji yangu na mke wangu huku wakidhani kuwa mimi ni kakake.

Tumekubaliana kufanya hivi huku mke wangu akihitajika kuwa mwangalifu asishike mimba za hawa madume wala kuwazia suala la ndoa.

Tuliamua kufanya hii kazi baada ya kujaribu kutafuta ajira kwa miaka bila mafanikio na kutokana na kuwa tulikuwa tunapendana na hatungeachana kwa sababu ya ufukara, tulitafuta mbinu mbadala kujipatia riziki.

Kupitia kazi hii tumefanya mambo kadha ikiwa ni pamoja na kununua majumba mawili ya kifahari jijini Nairobi na Mombasa, bali na kununua magari kadha na kuwapeleka watoto wetu katika shule za kifahari.

Sasa tumeanza kupanga mikakati ya kuwekeza ili angaa tutulie kama familia”.

You can share this post!

Buda taabani kufanyia yaya karamu ya bethidei

Shirika lasaka wanaume 100 kushiriki mpango wa kupanga uzazi

adminleo