• Nairobi
  • Last Updated March 19th, 2024 8:55 AM
Cositany amrukiaTuju vikali katikamzozo wa Jubilee

Cositany amrukiaTuju vikali katikamzozo wa Jubilee

 Na PATRICK LANG’AT

UBABE ndani ya chama tawala cha Jubilee unaendelea kutokota, Naibu Katibu Mkuu Caleb Kositany akimshutumu Katibu Mkuu Raphael Tuju kuhusiana na mabadiliko aliyolenga kutekeleza kwa maafisa wa kitaifa wanaosimamia chama hicho.

Bw Kositany ambaye pia ni mbunge wa Soy, kwa mara ya pili ndani ya siku tano, alimshambulia Bw Tuju akipuuza taarifa aliyotuma kwa wanachama awali akitoa ufafanuzi kuhusu mabadilko hayo.

Uhasama kati ya Mabw Tuju na Kositany umefasiriwa na wadadisi wa kisiasa kama wa Rais Uhuru Kenyatta na naibu wake William Ruto. Bw Tuju ni mwandani wa Rais huku Bw Kositany akirindimisha ngoma ya Dkt Ruto ya kuingia ikuluni mnamo 2022.

Kupitia taarifa jana, Bw Kositany aliwataka wanachama wa Jubilee kupuuza mabadiliko aliyoyasema yanasukumwa na Bw Tuju pamoja na Mwenyekiti wa Jubilee Nelson Dzuya kutimiza ajenda zao za kibinafsi.

‘Wanachama wa Jubilee wakiwemo viongozi wanafaa wapuuze taarifa zinazotolewa mara kwa mara na Bw Tuju. Jubilee ni chama kinachozingatia demokrasia na wazo la kila mwanachama linathaminiwa,’ akasema Bw Kositany kupitia taarifa kwa wanachama wote.

Mbunge huyo alitoa wito kwa Rais Kenyatta na Dkt Ruto kutumia mamlaka yao kuitisha kikao cha Kamati ya Kitaifa inayosimamia chama (NMC) akisema Bw Tuju amekataa au hana nia ya kuitisha kikao hicho.

‘Katibu Mkuu amekataa kuandaa mkutano wa NMC na kiongozi wa chama au naibu wake anafaa kuandaa kikao hicho. Hiyo itasaidia kuzima tofauti zinazoibuka ndani ya chama,’ akaongeza.

Mnamo Jumapili, Bw Kositany alikuwa ameamrisha kuwa Jubilee iandae uchaguzi wake baada ya janga la corona kutokomezwa.

Uchaguzi huo utaisaidia chama kuwachagua maafisa wa kudumu kwa kuwa wa sasa walipokezwa nyadhifa hizo 2017 ili wazishikilie kwa muda.

Kwenye mabadiliko aliyoyapendekeza Bw Tuju, maafisa waliotemwa ni Veronica Maina, Fatuma Shukri na Pamela Mutua.

Tuju, ambaye ni mbunge wa zamani wa Rarieda, aliwateua Lucy Nyawira Macharia, Profesa Marete Marangu, Walter Nyambati, Jane Nampaso na James Waweru kujiunga na NMC.

Kwenye taarifa fupi kwa wanachama, Bw Tuju alisema kuwa mabadiliko hayo yalichochewa na barua kutoka kwa Msajili wa Vyama, Bi Ann Nderitu ambaye alitoa mwongozo wa kufuatwa na chama kuandaa uchaguzi wa maafisa wake.

Kura hiyo ilifaa kuandaliwa mnamo Machi lakini ikaahirishwa hadi baadaye kutokana na janga la corona . Hata hivyo, kwenye barua ya jana, Bwa Kositany alisema Bi Maina, Shukri na Mutua hawajawahi kuwa wanachama wa NMC kwa hivyo kuondolewa kwao kulisukumwa na ajenda fiche ya kisiasa.

Aidha, Bw Kositany alipinga kwamba mkutano wa NMC uliandaliwa Februari 10 akisema wakati huo taifa lilikuwa likimwomboleza Rais Mstaafu marehemu Daniel arap Moi.

Wakati huo huo Kiongozi wa Wengi kwenye Bunge la Seneti Kipchumba Murkomen naye anataka maamuzi yote yaliyokuwa yametolewa na Bw Tuju miezi michache iliyopita, yabatilishwe na kuanguliwa upya.

‘Katibu wa Jubilee amekuwa akiendesha chama kama mali yake ya kibinafsi. Niliona barua zikiandikwa kwa mabunge ya kaunti ya Kirinyaga, Nairobi na Kajiado. Tuju alipata mamlaka wapi ya kuandika barua hizo? Kuanzia leo barua yoyote inayoandikwa lazima iidhinishwe na vitengo vyote vya uongozi wa chama,’ akasema.

You can share this post!

Ang’olewa paa la nyumba kwa kuchelewa kulipa kodi ya...

Walibora alitabiri kifo chake

adminleo