• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 7:00 PM
Mkurugenzi wa Skyways, wazazi wawatunuka walimu chakula na bidhaa muhimu

Mkurugenzi wa Skyways, wazazi wawatunuka walimu chakula na bidhaa muhimu

Na MISHI GONGO

IMEKUWA furaha kwa walimu wa shule ya msingi ya mmiliki binafsi ya Skyways iliyoko VOK eneobunge la Nyali baada ya wazazi na mkurugenzi wa shule hiyo kuwatunukia walimu chakula na bidhaa nyingine muhimu.

Wamesema ufadhili huo ni wa kuwasaidia walimu na wafanyakazi katika shule hiyo wakati huu ambapo shughuli nyingi za kiuchumi zimesitishwa.

Mkurugenzi wa shule hiyo Bi Dorothy Oloo amesema waliamua kuchukua hatua hiyo ili kuwasaidia ‘mzigo wa maisha’ walimu wake.

Bi Oloo amesema mchango huo uliongozwa na wazazi kama shukurani kwa walimu hao.

“Wazo hili lilitoka kwa wazazi; tulifaulu kuchanga pesa kisha tukawanunulia vyakula kama unga wa ngano, unga wa sima, mafuta ya kupikia, mchele, sabuni, sodo na bidhaa nyinginezo,” amesema.

Bi Oloo aidha amewashauri wakuu katika kampuni mbalimbali nchini kuweka mikakati itakayowasaidia wafanyakazi wao wakati huu mgumu.

Amesema wafanyakazi wengi wamekuwa wakipitia hali ngumu ya maisha tangu kuingia kwa ugonjwa wa Covid-19 nchini.

Chakula na bidhaa nyinginezo muhimu. Picha/ Mishi Gongo

Mzazi mmoja, Bi Halima Fadhili, amesema wamefanya hivyo kama njia ya kutoa shukurani zao kwa walimu hao kwa kuwaangalilia watoto wao.

“Tumeamua kuwakumbuka walimu wetu katika hali hii ngumu, tunawashauri wazazi wengine kuiga na kuwatunuku walimu wao pia na wasiojiweza katika jamii,” amesema mzazi huyo.

Machi 15, 2020, serikali ilitangaza kufungwa kwa shule zote nchini ili kudhibiti virusi vya corona.

Hali hiyo imesababisha baadhi ya walimu katika shule za wamiliki binafsi kukatwa mishahara kama njia ya kuziwezesha shule hizo kuendelea kujimudu.

You can share this post!

Mwanamke wa ‘simu ya kifo’ kutafutiwa wakili na...

Baadhi ya wakazi washutumu hatua ya serikali kuufunga Mji...

adminleo