• Nairobi
  • Last Updated March 19th, 2024 1:13 PM
Afisa wa serikali apondwa kutangatanga akijipigia debe kwa miradi ya maji

Afisa wa serikali apondwa kutangatanga akijipigia debe kwa miradi ya maji

 

NA MWANGI MUIRURI

KATIBU katika Wizara ya Maji Joseph Wairagu ameteswa na wanasiasa katika Kaunti ya Murang’a kwa madai ya kutumia miradi ya serikali kujipigia debe akilenga kutwaa ugavana wa kaunti hiyo 2022.

Analaumiwa kuweka mabango ya kuelezea miradi ya maji ambayo serikali inazindua katika kaunti hiyo yakiwa na maandishi bunifu ya kumpa umaarufu miongoni mwa wapiga kura wa Murang’a.

Katika kibango kimoja kilicho katika eneo la Nginda katika Kaunti Ndogo ya Maragua na ambacho kimezua malalamishi tele, Bw Wairagu amejiweka kama mwajiri wa mradi huo wa maji ya Maragua na ambao ulizinduliwa miezi mapema mwaka huu na Waziri wa Usalama wa ndani, Dkt Fred Matiang’i.

Wanaongoza kampeni zake katika eneo hilo wamezindua hatrakati za kusajili vibarua katika mradi huo wakliwaambia Bw Waioragu ndiye mwaajiri wao ilihali mwanakandarasi Sinohydro kutoka Uchina ndiye mwenye hela za kulipa.

“Mimi ninashindwa ni nini kinamsumbua huyu mfanyakazi wa serikali. Anarandaranda hapa Murang’a akiweka mabango yaliyo na jumbe za kupotosha akilenga kujipa umaariufu wa bwerere badala ya azingatie kazi aliyopewa na Rais Uhuru Kenyatta,” akateta gavana Mwangi wa Iria.

Alimkumbusha Bw Wairagu kuwa ni hatia katika sheria za uchaguzi kujipigia debe kisiasa ukitumia rasilimali za serikali.

Hata hivyo, Bw Wairagu amejipa uungwaji mkono wa Seneta wa Murang’a, Irungu Kang’ata ambaye aliambia Taifa Leo kuwa “sioni shida kubwa kwa Wairagu kujiangazia kama mwenye miradi hiyo.”

Alisema kuwa kwa sasa Wairagu akiwa ndiye Katibu maalum wa maji anafaa kupewa fursa ya kusambaza miradi Murang’a bila kukwamizwa na masuala ya tetesi kuhusu mabango.

“Mimi sijaona shida kubwa katika hali hii…tuzingatie kupata maji wala sio maandishi katika mabango,” akasema.

Bw Kang’ata ambaye pia analenga kuwania ugavana wa Murang’a 2022 hushirikiana na Wairagu katika ziara za Kaunti kukagua miradi na husemwa kuwa huenda wakawania pamoja, mmoja akiwa Naibu gavana.

Wengine ambao wamejikusanya pamoja kuwania ugavana wa Kaunti hiyo ambapo Wa Iria atastaafu 2022 baada ya kuhudumu kwa miaka 10 ni aliyekuwa mbunge wa Kigumo, Jamleck Kamau.

Kamau aliwania ugavana 2017 lakini akashindwa na Wa Iria katika mchujo wa Jubilee.

Katika mrengo wa Kamau kuna Mkurugenzi wa Shirika la Ahadi Kenya, Stanley Kamau, aliyekuwa Seneta wa Murang’a Kembi Gitura na aliyekuwa Naibu Gavana Gakure Monyo.

Wote wamesema kuwa wangetaka kampeni za wadhifa huo zizingatie sheria na kusiwe na wengine ambao watakiuka masharti ya uchaguzi ili kujipa guu mbele.

“Sisi tungependa sana serikali ya Rais Uhuru Kenyatta iafikie malengo yake ya kimaendeleo hasa katika safu ya usambazaji maji mashinani. Lakini hatutaki kuwe na mmoja wetu ambaye atapinda au avunje sheria ili ajipe umaarufu wa miradi ya rais,” wakasema katika taarifa ya pamoja Wikendi iliyopita wakiwa katika hospitali ya Kiria-ini walipopeleka misaada ya chakula na mavazi spesheli ya madaktari katika mapambano na janga la Covid-19.

You can share this post!

Howe aishusha Bournemouth daraja kisha ang’atuka

Victor Osimhen mwanasoka ghali zaidi Ulaya Mwafrika

adminleo