• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 1:29 PM
Atwoli akana kutoroka na mke wa watu

Atwoli akana kutoroka na mke wa watu

VICTOR OTIENO na PETER MBURU

KATIBU Mkuu wa muungano wa vyama vya wafanyakazi (COTU) Francis Atwoli amejitokeza kujibu uvumi uliotokea hivi majuzi kuwa alimnyanganya mwanamume mwingine mkewe, akisema kamwe hawezi kufanya hivyo.

Akizungumza mjini Kisumu jana, Bw Atwoli alipinga madai kuwa alitoroka na mke wa wenyewe (anayedaiwa kuwa msomaji wa habari za runinga), akisema alishauriwa na babake kutojihusisha na wake za watu.

Bw Atwoli alisema kabla ya kuoa mke mwingine, ni hulka yake kufika kwa wazazi na kutaka kujua ikiwa ameolewa ama yuko huru.

“Kuna mtu hivi majuzi alijaribu kuniharibia jina kuwa nilitoroka na mkewe, ni mwanaume mpumbavu wa aina gani, babangu alinishauri kuwa niwapo uhai nisicheze na wake za watu na hivyo siwezi kufanya hivyo,” akasema Bw Atwoli.

Katibu huyo alisema hata wake wengi aliooa hadi sasa, amekuwa akifuata taratibu zinazofaa kuhakikisha si wake wa wenyewe.

“Jamaa huyu hana akili timamu. Hata wake kadhaa nilio nao nimekuwa nikihakikisha kutoka kwa wazazi wao ikiwa wana wenyewe au la kabla sijawasilisha posa,” akasema Bw Atwoli.

Alisema kuwa babake alimshauri akitaka kuishi maisha marefu asiwahi kucheza na wake za watu.

Hii ilikuwa baada ya tetesi kuibuka kutoka kwa mwanasiasa kutoka eneo la Magharibi kuwa kiongozi huyo wa wafanyakazi alimnyanganya mke na kumtishia kumchukulia hatua kali.

 

You can share this post!

Kimombo kilimpiga chenga mfanyakazi wetu, Chandarana...

Wabunge walalamikia kuachwa kwa mabwanyenye ndani ya Mau...

adminleo