Na WANGU KANURI
HUKU mgomo wa matatu ukiendelea kushuhudiwa maeneo tofauti nchini Jumatano, Julai 12, 2023 magari katika kituo cha mabasi cha Makongeni, Thika yalipiga foleni huku wasafiri wakiadimika.
Hali hiyo iliashiria kinaya ambapo siku za kawaida abiria ndio hupanga laini ndefu kusafiri.
Msimamizi wa mabasi ya Supermetro, Amos Waweru alisema kuwa kwa kawaida wasafiri huwa wamepiga foleni wakisubiria magari lakini Jumatano ilikuwa siku ya aina yake.
“Kazi ya leo si nzuri hata kidogo. Magari ni mengi kuliko watu. Kutoka saa kumi na moja asubuhi hakujakuwa na wasafiri wengi kama kawaida,” akasema.
Wakati Taifa Leo Dijitali ilizuru kituo hicho mwendo wa saa tatu kasorobo, Bw Waweru alisema kwa kawaida ifikapo saa hizo, angalau magari 40 huwa yamebeba ila 20 pekee ndiyo yalikuwa yamebeba abiria.