Wakazi wa Nairobi wakosa maji, siku saba baada ya mafuriko
WAKAZI wa mitaa kadhaa jijini Nairobi wanakabiliwa na uhaba mkubwa wa maji baada ya mabomba ya kusambaza maji kuharibiwa na mafuriko yaliyosababishwa na mvua kubwa mnamo Ijumaa (Machi 6, 202) wiki jana.
Miongoni mwa mitaa inayoshuhudia uhaba wa bidhaa hiyo muhimu, kwa juma moja sasa, ni Buruburu Phase 1 na Phase, Kariobangi South na North, Dandora Phase 1, Mathare, Huruma na Eastleigh Section 3.
Katika mtaa wa Kariobangi South wakazi tuliowahoji walilalamika kuwa wanalazimika kununua maji, kutoka kwa wachuuzi, kwa bei ya hadi Sh50 kwa mtungi wa lita 20, hali inayowaongea mzigo wa gharama ya maisha.
“Tumeteseka zaidi tangu Jumamosi wiki iliyopita maji yalipokatika baada mvua kubwa kunyesha na tukaambiwa kuwa iliharipu paipu za kusambaza maji katika mtaa wetu. Sasa watu wa mkokoteni wanatuuzia maji kwa kati ya Sh40 na 50 kwa mtungi wa lita 20, maji ambayo hatujui kama ni salama au la,” akaeleza Bi Melisa Akinyi, mama wa watoto wawili.
“Kwa hivyo, kila siku mimi hulazimika kutumia karibu Sh200 kando na gharama ya kawaida. Tunaomba kampuni ya Maji ya Nairobi iharakishe ukarabati wa paipu zake ili tupate maji kama kawaida,” akaongeza mama hiyo ambayo ni mfanyabiashara katika soko la wazi la Gikomba.
Naye John Macharia ambaye ni mkazi wa Huruma alisema siku hizi yeye hukaa siku mbili bila kuoga kutokana na uhaba wa maji.
“Nikinunua lita 20 ya maji mimi huitumia siku mbili kupikia na kuosha vyombo vya jikoni. Sijafugua nguo Jumamosi wiki jana, siku ambayo maji yalikatika na siku hiyo nalazimika kukaa siku mbili bila kuoga,” anaeleza mchuuzi huyo ambaye anaishi pekee yake.
“Tutapata magonjwa hatari hali ikiendelea hivi. Tunaomba kampuni ya maji iharakishe kutengeneza paipu zao ili tupate maji kama mawaida,” akaongeza.
Mnamo Jumamosi wiki jana Kampuni ya Maji na Majitaka ya Nairobi (NCWSC) ilitoa taarifa ikielezea kuwa jumla ya mitaa 15 ingekosa maji baada ya mabomba yake kuharibiwa na mafuriko yaliyosababishwa na mvua kubwa iliyoshuhudiwa siku iliyotangulia.
“Kampuni ya Maji ya Nairobi ingependa kuwajulisha wateja wake kwamba mvua kubwa iliyoshuhudiwa usiku wa jana (Ijumaa, Machi 6, 2026) na mafuriko yaliyotokea yameharibu mabomba kadhaa ya kusambaza maji. Kwa hivyo, usambazaji wa maji umekatiza katika jumla ya mitaa 15, haswa ile iliyoko mashariki mwa Nairobi,” kampuni hiyo ikaeleza.
Ilieleza kuwa mabomba makuu yaliyoharibiwa ni pamoja na bomba lililoko kwenye barabara ya Outering katika kivuko cha Mto Nairobi, bomba la Easleigh-Kiambiu, bomba la Korogocho-Dandora na bomba la eneo la Brookside Drive.
Mitaa mingine iliyoathirika ni; Jerusalem, Uhuru, Jericho, Ofafa, Harambee, Korogocho,Kiambiu, Mathare na Lower Kabete Lane.
NCWSC iliwahakikishia wakazi katika mitaa iliyoathirika kwamba wahandisi wake wako mbioni kurekebisha mabomba yaliyoharibika na mafurika “ili kurejesha huduma za usambazaji maji haraka iwezekanavyo.”
Hata hivyo, siku sababu zimepita kabla huduma za kawaida za usambazaji wa maji kurejelewa.