Kimataifa

Amerika yaruhusu uuzaji wa mafuta kutoka Urusi Iran ikifunga Mkondo wa Hormuz

Na MASHIRIKA March 14th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

SERIKALI ya Amerika imeruhusu kwa muda uuzaji wa mafuta kutoka Urusi yaliyoko baharini, baada ya bei za nishati kupanda kutokana na vita vinavyoendelea katika eneo la Mashariki ya Kati.
Haya yanayojiri huku Iran ikiendelea kuushambulia Mkondo wa Hormuz.
Hatua hiyo inamaanisha kuwa Amerika italegeza kwa muda vikwazo vya kiuchumi dhidi ya Urusi.
Wizara ya fedha Amerika imetoa tangazo hilo jana ikiidhinisha usafirishaji na uuzaji wa mafuta ghafi ya Urusi na bidhaa nyingine za petroli zilizokwama baharini.
Waziri wa fedha wa Amerika, Scott Bessent, alisema idhini hiyo mpya inalenga kuongeza uwiano wa kimataifa wa upatikanaji wa mafuta, lakini akisisitiza kuwa hizo ni hatua za muda mfupi.
Vita vya Iran vimevuruga sekta za nishati na usafirishaji duniani na kusimamisha shughuli katika Mkondo wa Hormuz.
Inadaiwa kuwa hatua hiyo ilichukuliwa jana baada ya kiongozi mkuu mpya wa Iran, Ayatollah Mojtaba Khamenei, kuagiza njia muhimu ya safari za meli za mafuta ya Mkondo wa Hormuz iendelee kufungwa.
Khamenei, ambaye inadaiwa alijeruhiwa katika shambulizi la anga lililotekelezwa na Amerika ikishirikiana na Israeli, bado hajaonekana hadharani tangu kuteuliwa kwake Jumapili iliyopita kama kiongozi mkuu.
Khamenei pia ametaka mataifa ya Ghuba kufunga kambi za kijeshi za Amerika.
Haya yanajiri muda mchache tu baada ya ndege ya Amerika aina ya KC-135 kuanguka magharibi mwa Iraq, huku ndege ya pili iliyohusika katika tukio hilo ikifanikiwa kutua salama.
Kwa mujibu wa Kamandi kuu ya jeshi la Amerika, kanda ya Mashariki ya Kati CENTCOM, kuanguka kwa ndege hiyo hakujasababishwa na shambulio la adui, ingawa jeshi la Iran limedai katika taarifa yake kwamba kundi moja washirika wao nchini Iraq, ndio limeidungua ndege hiyo kwa kombora na kuua wafanyakazi wote.
KC‑135 ni ndege ya nne ya kijeshi ya Amerika kuanguka tangu vita hivyo vizuke, baada ya ndege tatu za F‑15 kuangushwa kwa bahati mbaya Kuwait.
Naye Waziri Mkuu wa Israeli, Benjamin Netanyahu alisema kuwa kampeni ya pamoja ya Amerika na Israeli inaendelea “kuikandamiza” Iran na kundi la wanamgambo la Hezbollah. Akizungumza kwenye televisheni, Netanyahu alisema vita dhidi ya Iran vinalenga “kuangusha na kuzima kabisa utawala wao,” pamoja na kudhoofisha programu zake za nyuklia na makombora.
Katika maelezo yake ya kina kuhusu vita, Netanyahu alisema kwamba anataka kutumia mzozo huo kuondoa madarakani utawala wa viongozi wa kidini mjini Tehran.