Kutakuwa na mvua na radi maeneo haya wikendi, idara yaonya
Idara ya Hali ya Hewa nchini (KMD) imewaonya Wakenya katika maeneo mbalimbali kujiandaa kwa mvua za wastani hadi kubwa kwa siku tano zijazo, kuanzia Ijumaa, Machi 27 hadi Jumanne, Machi 31.
Katika tahadhari yake, idara hiyo ilisema mvua kubwa inatarajiwa katika maeneo ya Kati, Magharibi, Bonde la Ziwa Victoria, Bonde la Ufa na Kaskazini Mashariki.
Kaunti zitakazoathiriwa katika maeneo ya Magharibi, Bonde la Ufa na Bonde la Ziwa Victoria ni pamoja na Siaya, Kisumu, Homa Bay, Migori, Kisii, Nyamira na Trans Nzoia. Nyingine ni Baringo, Uasin Gishu na Elgeyo Marakwet, huku hali kama hiyo ikitarajiwa pia Nandi, Nakuru, Narok, Kericho, Bomet, Kakamega, Vihiga, Bungoma, Busia na Pokot Magharibi.
Katika eneo la Kati, kaunti za Nyandarua, Laikipia, Nyeri, Kirinyaga, Murang’a, Kiambu, Meru, Embu, Tharaka Nithi pamoja na Nairobi zinatarajiwa kupokea mvua za wastani katika kipindi hicho.
Idara hiyo ilieleza kuwa maeneo mengi yatashuhudia hali ya jua na mawingu asubuhi, ikifuatiwa na mvua alasiri.
Katika maeneo ya Magharibi, Bonde la Ufa na Ziwa Victoria, mvua hiyo inaweza kuandamana na radi, huku wakazi wakionywa kuhusu hatari ya mafuriko.
Hali kama hiyo pia inatarajiwa katika kaunti za Pwani za Mombasa, Kilifi, Lamu na Kwale pamoja na eneo la Delta ya Tana, ambapo mvua ya wastani inatarajiwa kunyesha.
Hata hivyo, maeneo ya kusini mashariki mwa nchi yanatarajiwa kubaki na hali ya jua na kame kwa siku hizo tano.
Wakati huo huo, idara ya hali ya hewa imeonya kuhusu baridi kali usiku katika maeneo ya Kati, ambapo halijoto inatarajiwa kushuka hadi nyuzi joto 7 kiwango cha selsias.
Kaunti zitakazokumbwa na baridi hiyo ni Nyandarua, Laikipia, Nyeri, Kirinyaga, Murang’a, Kiambu, Meru, Embu, Tharaka Nithi na Nairobi.
Kwa upande mwingine, maeneo ya Pwani, Kaskazini Mashariki na Kaskazini Magharibi yanatarajiwa kushuhudia joto la zaidi ya nyuzi joto 30 wakati wa mchana.