Kimataifa

Trump asema viongozi wapya Iran ‘wana akili’

Na REUTERS March 31st, 2026 Kusoma ni dakika: 2

WASHINGTON/ISLAMABAD

RAIS Donald Trump kwa mara nyingine amesema kuwa Amerika na Iran zimekuwa zikifanya mikutano “ kwa njia ya moja kwa moja na isiyo ya moja kwa moja” huku akiwataja viongozi wapya wa Iran kama “wenye kutumia akili zao vizuri”.

Alisema hayo wakati ambapo wanajeshi wa Amerika waliwasili Mashariki ya Kati na Iran ikaonya kuwa haitakubali kukandamizwa.

Kauli ya Trump aliyoitoa Jumapili ilijiri baada ya Pakistan, inayotekeleza wajibu wa mpatanishi kati ya Iran na Amerika, kusema inajiandaa kuandaa “mazungumzo ya maana” katika siku zijazo kwa lengo la kukomesha vita ambavyo vimedumu kwa mwezi mmoja.

“Nadhani tutafikia muafaka na wao. Nina uhakika, lakini pia kuna uwezekano kwamba huenda tusikubaliane,” Trump akawaambia wanahabari Jumapili jioni alipokuwa akisafiri kwa ndege yake rasmi, (Air Force One) kuelekea Washington.

Rais huyo alisema alidhani kuwa Amerika imefaulu kubadilisha uongozi nchini Iran baada ya kutekeleza mashambulio yaliyomuua kiongozi wake mkuu na viongozi wengine, lakini akaelezea kuwa waliochukua nafasi zao wanaonekana “wazuri kiakili.”

Shambulio la kwanza lililotekelezwa na Israeli na Amerika Februari 28 liliua Kiongozi wa Kidini wa Iran Ayatollah Ali Khamenei, ambaye nafasi yake ilijazwa na mwanawe wa kiume Mojtaba.

Vita hivyo vimeenea katika mataifa kadhaa ya Mashariki ya Kati, Iran ikitekeleza mashambulio ya kulipiza kisasi dhidi ya vituo vya Amerika, na kusababisha vifo vya maelfu ya watu.

Mapigano hayo yamevuruga shughuli za usafirishaji mafuta na bidhaa nyinginezo, hali ambayo imeathiri uchumi wa ulimwengu.

Waziri wa Masuala ya Kigeni wa Pakistan Ishaq Dar amesema mazungumzo kati ya mawaziri wa kigeni wa mataifa ya ukanda huu Jumapili yalihusu njia za kukomesha vita hivyo.

Aidha, walijadili mipango ya kuandaliwa kwa mazungumzo jijini Islamabad kati ya wajumbe wa Amerika na wa Iran.

“Pakistan itapewa nafasi ya kuwa mwenyeji na msimamizi wa mazungumzo kati ya pande hizo mbili katika siku zijazo kwa lengo la kupata muafaka wa kukomesha vita vinavyoendelea,” Ishaq akasema.

Haikujulikana wazi ikiwa Amerika na Iran zimekubali kutuma wajumbe kuhudhuria mkutano huo.

Awali, Spika wa Bunge la Iran Mohammad Baqer Qalibaf aliikashifu Amerika kwa kutuma jumbe kuhusu uwezekano wa kufanyika kwa mazungumzo huku ikipanga mashambulio ya ardhini.

Spika huyo alisema Iran iko tayari kujibu ikiwa wanajeshi wa Amerika wataletwa.

“Mradi Waamerika wanataka Iran ikubali kushindwa, jibu letu ni kwamba katu hatutakubali kukandamizwa,” Spika Qalibaf akaeleza kwenye ujumbe kwa taifa.

Wizara ya Ulinzi nchini Amerika iliwatuma maelfu ya wanajeshi katika eneo la Mashariki ya Kati, ikimpa Trump nafasi ya kuamuru kuanzishwa kwa mashambulio ya ardhini.

Afisa mmoja wa Israeli alisema hakuna nia ya kupunguzwa kwa mashambulio dhidi ya Iran kabla ya mazungumzo yoyote kati ya Amerika na Iran na kwamba Israeli itaendelea kutekeleza mashambulio katika vituo vya jeshi la Iran.

Jeshi la Ulinzi la Israel (IDF) lilisema limetekeleza mashambulio 40 ya angani katika maeneo ya kari na magharibi mwa Iran, ikiwemo jiji kuu Tehran, ndani ya saa 24 hadi Jumapili jioni.

Lilidai kushambulio vituo vya kurusha makombora, maghala ya kuhifadhi silaha miongoni mwa vituo vingine.