Habari

RUTO: Tanzania, Uganda, Rwanda si ligi yetu, tuko mbele kimaendeleo

Na KEVIN CHERUIYOT April 20th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

RAIS William Ruto amewataka wakosoaji wake wakome kulinganisha bei ya mafuta nchini na mataifa jirani akisema uchumi wa Kenya umepiga hatua na unastahili kufananishwa na nchi zenye mapato ya wastani.

Wakenya na viongozi wa upinzani wamekuwa wakikashifu serikali kutokana na bei ya juu ya mafuta ikilinganishwa na Uganda, Tanzania, Rwanda, Sudan Kusini, Burundi na nchi nyingine za ukanda wa Afrika Mashariki (EAC).

Hii ni licha ya kuwa baadhi ya nchi hizo huyapata mafuta yao kupitia Bandari ya Mombasa ilhali huyauza kwa bei ya chini ikilinganishwa na Kenya.

Kwa sasa bei ya lita moja ya petroli ni Sh197.6, dizeli Sh196.6. Hii ni baada ya vilio vya Wakenya kumlazimisha Rais kupunguza ushuru wa VAT kutoka asilimia 13 hadi nane. Kabla ya hapo ushuru huo ulikuwa asilimia 16.

Vilio vya Wakenya vilianza Aprili 15 baada ya mamlaka ya kawi na petroli (EPRA) kutangaza bei mpya za petroli (Sh206.97) na dizeli (Sh206.84)
Uganda ambayo hutegemea sana Bandari ya Mombasa huuza lita ya petroli kwa Sh184.55 na dizeli kwa Sh174.10 hali Tanzania lita ya petroli ni Sh189.81 kisha dizeli ni Sh189.11.

Bei ya chini zaidi katika ukanda huu wa Afrika iko Ethiopia ambapo lita moja ya petroli ni Sh109 kisha dizeli ni Sh115.70.

Rwanda lita ya petroli ni Sh203.17 kisha dizeli ni Sh194.52.

Jana, Rais alisema uchumi wa Kenya ndio ‘babalao’ Afrika Mashariki hivyo basi haufai kulinganishwa na jirani zake.

“Kenya imefikia nchi ambazo zina mapato ya wastani ilhali jirani zetu bado ni kati ya mataifa yanayoendelea. Ukitaka kulinganisha Kenya, basi limganisha na nchi zenye uchumi wa kadri na hapa ndipo utapata takwimu sahihi,” akasema Rais Ruto.

“Nchi zilizo katika kundi la uchumi wa wastani zina bei ya mafuta sawa na sisi,” akasema na kuongeza kuwa Kenya inatumia maelfu ya pesa kugharimia ujenzi wa maelfu ya kilomita ya miundomsingi mipya, jambo ambalo majirani hawalifanyi.

“Kodi za mafuta yetu ndizo hugharimia miundomsingi yetu. Wakenya wanastahili kujua kuwa tuna kilomita 20,000 za barabara za lami zinazohitaji matunzo na kilomita nyingine 6,000 za barabara inayowekwa lami.

Ukijumuisha takwimu za Uganda, Tanzania, DR Congo, Rwanda, Burundi na Sudan Kusini, barabara zao zilizojengwa hazifiki hata kilomita 20,000,” akasema.

Alikuwa akiongea jana katika ibada ya kanisa la PAG mtaani Karen, Nairobi akiwa ameandamana na viongozi wa ngazi mbalimbali za serikali.

“Kilomita 20,000 za lami tulizonazo ni nyingi kuliko barabara ambazo zimewekwa lami katika mataifa saba jirani katika ukanda wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC). Kilomita 6,000 tunazojenga sasa ni sawa na kiasi cha barabara ambazo zimewekwa lami kwa miaka 60 katika nchi hizo jirani,” akasema.

Matamshi ya Rais yanajiri huku upinzani wiki jana ukitishia kuongoza maandamano kutokana na bei za juu za mafuta.

Viongozi na makundi mbalimbali ya vijana yamekuwa yakisukuma serikali ipunguze bei ya mafuta iwapo haitaki maandamano.

Katika ibada ya jana mtaani Karen, Kiongozi wa Wengi, Kimani Ichung’wah alipuuzilia mbali vitisho vya aliyekuwa Naibu wa Rais Rigathi Gachagua vya kuongoza maandamano wiki hii akisema hilo haliwezi kupunguza gharama ya mafuta.

“Nikiwasikia watu wakisema watasimamisha shughuli jijini Nairobi kupitia maandamano, huwa ninashangaa. Unasaidikaje ukiwatishia Wakenya kuwa utazua ghasia na kufunga Nairobi kwa sababu ya bei ya mafuta? Hii itazidisha tu hali mbaya,” akasema Bw Ichung’wah.

Waziri wa Usalama wa Ndani Kipchumba Murkomen ambaye pia alihudhuria ibada hiyo aliwalaumu wanasiasa akisema ndio tishio kwa usalama wa taifa kwa sababu wanawadhamini vijana kushiriki uhuni wa kisiasa.

“Tutaendesha oparesheni kali ya kuwandamana wahuni hawa na wiki jana, tuliwakamata vijana 100 wanaotumiwa na wanasiasa Nairobi. Wiki jana kule Kitale, tuliwanasa vijana 200 ambao wanashiriki uhuni,” akasema Bw Murkomen.