Habari Mseto

Familia yasaka Sh2m kuokoa jamaa anayezuiliwa na maafisa wa Trump nchini Amerika

Na DAVID MONDA April 27th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

FAMILIA ya Mkenya aliyezuiliwa katika Idara ya Uhamiaji Amerika, ICE, inajikakamua kukusanya Sh2 milioni kumwezesha aachiliwe huru akisubiri kesi dhidi yake iliyopangiwa kusikizwa Mei 4.

Cyrus Thairu, ni mhamiaji Mkenya aliyeenda Amerika kwa cheti cha usafiri cha B2, ambacho muda wake ulikamilika na kumfanya mhamiaji haramu.

Wahamiaji wasioidhinishwa wanafafanuliwa na Wizara ya Usalama wa Ndani Amerika kuwa “watu wote wasio raia waliozaliwa katika nchi za kigeni na ambao si wakazi rasmi.”

Idadi kubwa ya wahamiaji haramu huingia Amerika ama bila kukaguliwa au walipatiwa kibali cha muda na wakaendelea kuishi baada ya tarehe waliyohitajika kuondoka.

Cyrus yupo katika kitengo hikii Amekuwa kizuizini tangu Machi 26, na amewasilisha kesi kuomba hifadhi ya uhamiaji na ICE katika Jimbo la Illinois.

Dereva huyu wa trela alikuwa anasafirisha mizigo kutoka Illinois kuelekea Texas na alipokuwa akirejea New York, Machi 26, 2026, alisimamishwa na maafisa wa uhamiaji katika kituo cha ukaguzi karibu na mpaka na Mexico.

Aliwekwa kizuzini na ICE na anakabiliwa na kesi ya kumrejesha kimabavu nchini.

Dada yake, Joyce Thairu, anasema familia yake imeajiri wakili wa uhamiaji, Irene Mugambi, kumtetea Cyrus.

Wanajaribu kukusanya Sh2 milioni kuwezesha aachiliwe huru kabla ya kesi yake kusikizwa.

Akizungumza kwa simu jijini Seattle Washington, Joyce alisema: “ICE imemzuilia Cyrus. Amekuwa kizuizini kwa zaidi ya mwezi mmoja sasa. Ni kipindi kigumu mno kwa familia yetu. Dada yangu Mary Thairu amesafiri Texas kumshughulikia Cyrus na kuzungumza na wakili wake Irene Mugambi.”

“Familia yetu inajaribu kukusanya Sh2 milioni kuwezesha aachiliwe huru kabla ya kesi yake Mei 4. Kama hatutaweza kukusanya kiasi hicho cha dhamana, itabidi asalie katika kizuizi cha ICE. Jamii ya Wakenya inahofia maslahi yake kwa sababu ana mke na watoto Kenya na yuko katika vituo hatari korokoroni.”

Kulingana na wakili wa uhamiaji, Blaise Odhiambo, Ubalozi wa Kenya unaweza kusaidia kwa kumwezesha kupata wakili iwapo angehitajika.

“Wakili wa familia yake atalazimika kuwasiliana na ubalozi na kuwafahamisha kuhusu hadhi yake.”

Kwa bahati mbaya, watu wengi wanaosaka hifadhi kama Cyrus, hujipata korokoroni wakisubiri maamuzi ya kesi zao.

Texas ni jimbo la wanajadi ambapo Gavana wake, Greg Abbott, amechukua msimamo mkali kuhusu wahamiaji haramu katika Jimbo hilo huku akichangia pakubwa kampeni kali dhidi ya uhamiaji.