Akili Mali

‘Nyama ya bata ni tamu’: Jinsi ufugaji wa mabata unalipa ukifanywa vyema

Na JOHN NJOROGE May 6th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

SUSAN Wairimu Kamau, ni mfugaji mabata aina ya Muscovy katika eneo la Elburgon, Kaunti ya Nakuru.

“Mwaka wa 2020, nilishawishiwa kuanza kilimo hiki cha kufuga mabata na rafiki yangu ambaye aliwalea kwa wingi. Mkulima huyo alikubali kuniuzia bata dume na jike kwa Sh800 kila mmoja. Kwa Sh5,000 nilizokuwa nazo kama mtaji, nilitumia salio la fedha hizo kwa kujenga nyumba ya mabata hao,” anasema Wairimu, akiongeza kuwa baada ya mwezi mmoja, bata alianza kutaga mayai.

Baaada ya mwezi mwingine mmoja wa kutaga mayai, mchakato wa kuangua mayai ulikuwa ukiendelea. Anasema bata hufunika mayai kwa manyoya laini hadi vifaranga waanguliwe.

Wairimu anaeleza kuwa baada ya siku 28, alishangaa kuona vifaranga wote 20 kutoka kwa mayai yote yaliyofunikwa kwa manyoya yakianguliwa bila hata moja kupotea ama kukosa kuanguliwa kutoka kwa mayai hayo ikilinganishwa na kuku ambao kwa mara nyingi si mayai yote huanguliwa vifaranga.

Wairimu anasema siku chache baada ya kuanguliwa, vifaranga hao walianza kumfuata mama kwa ajili ya kupata lishe na maji.

Anasema kundi la kwanza la vifaranga hao lilimpa motisha ya kupanua na kujenga jengo lingine ambalo lilikuwa kubwa ili kuwatosha bata na vifaranga wote kwa jumla.

“Niliendelea kuwa na usimamizi na uangalizi mzuri wa kundi langu kwa kuwapa mboga za kijani na malisho mengine. Ikilinganishwa na kuku, mabata hutaga mayai mengi zaidi na wana nafasi kubwa ya kuangua yote. Siwezi kuwa na majuto kuanza kilimo hiki kwani kimeniwezesha kulipa karo kwa watoto wangu na kukidhi mahitaji mengine ya msingi kutokana na mauzo,” anasema Wairimu, akiongeza kuwa soko la mabata na mayai katika eneo hilo ni zuri na lenye wateja wengi ambao hajaweza kufikia mahitaji yao.

Mapato

Idadi ya kundi la mabata linapoongezeka, mkulima huwauza katika soko la ndani kulingana na ukubwa wao.

Bata jike wa Muscovy aliyekomaa huuzwa kwa Sh1,300 na dume kwa Sh1,500 kwa kila mmoja.

Yai moja anauza kwa Sh50 huku trei yenye mayai 30 akiuza kwa Sh1,500.

Katika mwaka wa 2021, mkulima huyu anasema kuwa soko lilikuwa zuri kwani bata wake walifikia idadi ya 200. Aliuza kila bata aliyekomaa kwa kati ya Sh1,200 na Sh1,500 mtawalia kulingana na ukubwa.

“Kutokana na mauzo hayo, niliongeza kundi lingine, nikanunua chakula cha kutosha na nikatumia ya ziada kwa kulipia watoto wangu karo,” anaeleza, akiongeza kuwa kilimo hiki hakina madalali kwani wateja huja moja kwa moja kwa wakulima.

Mabata wa Muscovy waliendelea kuongezeka, kutaga mayai na kuangua vifaranga zaidi, hasa baada ya miezi miwili na nusu.

Wairimu alisema kuwa mpango wake kwa siku zijazo ni kuongeza aina hiyo ya mabata hadi 1,000 na kuwa mkulima anayeongoza katika eneo hilo licha ya gharama kubwa ya chakula.

Wakati wa kiangazi, anasema huwa na changamoto kuwafuga kwa sababu mboga za kijani kibichi, kabeji na vyakula vingine kutoka shambani ambazo wanapenda kula huwa chache.

Kwa sababu hii, anasema kuwa ni bora kuwafuga ndege hao wakati wa mvua ya wastani.

Kwa usalama wa kundi lake ambalo limezidi kongezeka polepole, mpango wake ni kujenga nyumba ya kisasa ambayo itahifadhi zaidi ya mabata 500 na kuhakikisha kwamba hawatakuwa katika hatari ya wizi, ambayo ndiyo changamoto kuu katika eneo hilo.

Mkulima huyu hujifunza mtandaoni jinsi ya kudumisha na kufanikisha kilimo chake na kupata vidokezo vya kudhibiti na kuzuia mashambulizi ya magonjwa ambayo anasema hayapatikani sana katika mabata wa kufugwa.

Anahimiza wakulima wengine chipukizi, kukumbatia kilimo hiki na kujipatia ajira kwani ni rahisi kuanzisha ukulima huu hata kwa sehemu ndogo.

Pia, anawaomba maafisa wa mifugo kupitia serikali ya kaunti kuandaa mabaraza kwa ajili ya wafugaji wa mabata kama inavyofanyika kwa wakulima wa nafaka na viazi ili kuboresha kilimo chao na kukifanya kiwe kizuri na cha bei nafuu kwa wakulima wote ambao wangetaka kuanzisha ukulima huu.