Kimataifa

Njama ya kumrefushia Mnangagwa urais yazua kilio Zimbabwe

Na REUTERS June 3rd, 2026 Kusoma ni dakika: 2

HARARE, Zimbabwe:

SERIKALI ya Zimbabwe mnamo Jumanne iliwasilisha mswada bungeni ambao utaongeza muda wa urais wa Rais Emmerson Mnangagwa kwa miaka miwili hadi 2030.

Mswada huo uliwasilishwa licha ya ukosoaji kutoka kwa upinzani uliogawanyika na baadhi ya viongozi wakongwe ambao walipigania uhuru wa taifa hilo.

Mswada huo ulitarajiwa kujadiliwa jana wakati ambapo ungesomwa kwa mara ya pili bungeni.

Mnangagwa, 83, anapaswa kuondoka madarakani 2028 baada ya kuhudumu mihula miwili ya miaka mitano kama kiongozi wa nchi.

Hata hivyo, wafuasi wake wanataka katiba ibadilishwe ili kuongeza muda wa muhula wa urais kutoka miaka mitano hadi saba.

Pia wanataka marais wachaguliwe na bunge badala ya kuchaguliwa moja kwa moja na wananchi kupitia kura ya umma jinsi ambavyo imekuwa ikifanyika.

Waziri wa Sheria Ziyambi Ziyambi, aliwasilisha mswada huo katika bunge na kuupigia debe.

Wachanganuzi wa masuala ya kisiasa wanatarajia mswada wenyewe kupitishwa kwa urahisi kwa kuwa chama tawala cha ZANU-PF cha Mnangagwa kina wingi wa theluthi mbili katika bunge la chini.

Pia ZANU-PF inadhibiti kwa kiwango kikubwa bunge la juu kupitia viongozi wa wakongwe na washirika wengine ambao kwa kawaida hupiga kura kukiunga chama hicho.

Hali hiyo inakipa chama hicho idadi ya kura zinazohitajika kufanya marekebisho hayo ya katiba.

Ziyambi hapo awali alinukuliwa akisema kuwa mchakato huo wa kubadilisha katiba unatarajiwa kuchukua zaidi ya mwezi moja.

Chama cha ZANU-PF kimetawala Zimbabwe tangu nchi hiyo ipate uhuru kutoka kwa Uingereza 1980.

Ilipata uhuru chini ya kiongozi wa muda mrefu Robert Mugabe na baadaye chini ya Mnangagwa, ambaye alichukua madaraka kufuatia mapinduzi mnamo 2017.

Jumanne, kundi la majenerali wastaafu na watumishi wa zamani wa umma lilitangaza hadharani upinzani wake dhidi ya mswada huo unaolenga kuongeza muda wa Mnangagwa madarakani.

Walisema walikutana na Mnangagwa mwezi uliopita kueleza wasiwasi wao, lakini kiongozi huyo aliwaambia waache sheria ichukue mkondo wake.

Baadhi ya waliopigania vita vya ukombozi na wanaharakati pia wameupinga mswada huo katika Mahakama ya Katiba ya Zimbabwe.

Hata hivyo, korti hiyo imeahirisha uamuzi wake huku ikiendelea kuzingatia hoja zilizowasilishwa na walalamishi.