Viongozi wa upinzani watua Magharibi kuuza sera
VIONGOZI wa upinzani Ijumaa walianza ziara ya siku tatu katika eneo la Magharibi mwa Kenya wakimshutumu Rais William Ruto kwa kile walichodai ni kusaliti jamii ya Waluhya baada ya kushindwa kutekeleza ahadi alizotoa kabla ya uchaguzi wa mwaka 2022.
Msafara huo unaongozwa na kiongozi wa chama cha Democracy for Citizens Party (DCP) Rigathi Gachagua, kiongozi wa Wiper Kalonzo Musyoka na Eugene Wamalwa wa Democratic Action Party of Kenya, huku ukijumuisha pia Justin Muturi, Cleophas Malala, Gavana wa Trans Nzoia George Natembeya, Mbunge wa Mumias Mashariki Peter Salasya na Seneta Gloria Orwoba.
Viongozi hao walizuru Luanda Khwirumbi, Khayega, Malava, Mayige na Shikomari wakitoa wito kwa jamii ya Waluhya kuungana na kusimamisha mgombea mmoja wa urais atakayepambana na Rais Ruto katika uchaguzi mkuu wa 2027.
Akizungumza katika soko la Luanda, Gachagua alionyesha nakala ya mkataba wa makubaliano uliotiwa saini kati ya Rais Ruto, Mkuu wa Mawaziri Musalia Mudavadi na Spika wa Bunge la Kitaifa Moses Wetang’ula kabla ya uchaguzi wa 2022.
Alidai katika mkataba huo, Rais Ruto uliahidi jamii ya Waluhya asilimia 30 ya nyadhifa serikalini pamoja na miradi ya maendeleo, lakini mengi hayajatekelezwa.
“Nilikuwepo wakati Ruto alipotia saini makubaliano hayo. Aliahidi Waluhya asilimia 30 ya serikali na maendeleo makubwa, lakini hajatimiza ahadi hizo,” alisema Gachagua.
Alisema miradi mingi iliyoahidiwa, ikiwemo kilomita 1000 za barabara za lami na kiwanda cha kusindika samaki, bado hazijatekelezwa huku viwanda vya sukari kama Mumias na Nzoia vikidaiwa kuuzwa badala ya kufufuliwa.
Gachagua pia alidai kuwa alipomuuliza Rais kuhusu ahadi ambazo hajatekelezwa kwa maeneo ya Mlima Kenya na Magharibi, alitishiwa kuondolewa madarakani.
Aliwahakikishia wakazi kuwa upinzani utakuwa na mgombea mmoja wa urais mwaka 2027 na kuwataka wasikubali ahadi za kuungwa mkono katika uchaguzi wa 2032.
Bw Malala aliwataka Waluhya kuungana na kuchagua msemaji wao ndani ya siku 45 zijazo, akionya kuwa iwapo waathiriwa wa maandamano hawatalipwa fidia kabla ya Juni 25, upinzani utaandaa maandamano makubwa nchini.
Bw Wamalwa alisema jamii ya Waluhya haijapata manufaa iliyotarajia kutoka serikali na badala yake viwanda vya sukari vimebinafsishwa huku miradi ya maendeleo ikikwama.
“Tumezunguka nchi nzima na tumeona kutoridhika kwa wananchi kunazidi kuongezeka kila siku.”