Habari

Serikali yatoa mapendekezo tele kwenye bajeti ‘kuwapanguza machozi Gen Z

Na Na KIMANI MWANGI June 13th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

VIJANA nchini ni miongoni mwa walionufaika zaidi katika bajeti ya mwaka wa fedha 2026/2027 iliyowasilishwa na Waziri wa Fedha, John Mbadi, huku serikali ikitenga mabilioni ya fedha kwa elimu, ajira, ubunifu wa kidijitali, michezo, makazi na mipango ya ustawi wa jamii ili kupunguza tatizo la ukosefu wa ajira.
Ukosefu wa ajira umeendelea kuwa changamoto kubwa nchini, huku maelfu ya wahitimu wakijiunga na soko la ajira kila mwaka lisilo na nafasi za kutosha za kazi.
Ili kukabiliana na hali hiyo, Wizara imependekeza zaidi ya Sh20 bilioni kwa mipango inayolenga kuwawezesha vijana moja kwa moja.
Huduma ya Kitaifa kwa Vijana (NYS) imetengewa Sh12.5 bilioni, mpango wa NYOTA Sh4.9 bilioni, Mpango wa Kusaidia Ajira kwa Vijana Sh1.6 bilioni na Huduma za Maendeleo ya Filamu Sh1 bilioni.
Mbadi alisema mpango wa NYOTA tayari umewapa vijana 51,604 nafasi za kupata uzoefu wa kazi katika kaunti 26 huku zaidi ya vijana 91,000 wakinufaika na ruzuku za kuanzisha biashara.
Aidha, serikali imetoa mikopo kwa vijana 93,559 kupitia Hazina ya Maendeleo ya Biashara kwa Vijana ili kuwasaidia kuanzisha na kukuza biashara ndogo ndogo.
Wizara pia imependekeza Sh2.4 bilioni kwa mpango wa Kenya Jobs and Economic Transformation unaolenga kukuza viwanda na kuunda nafasi zaidi za ajira.
Mbadi alisema serikali inaendelea kuimarisha ujuzi na uwekezaji wa vijana kupitia mafunzo, ushauri na upatikanaji wa mitaji ya biashara.
Katika sekta ya afya, mradi wa Vijana Vuka na Afya (ViVA) umefaulu kuwafikia vijana 72,623 katika Nairobi, Kisumu na Mombasa kwa kuwapatia huduma za afya ya uzazi kwa gharama nafuu, hatua inayolenga kuboresha ustawi wao na kuongeza uzalishaji.
Elimu ndiyo sekta iliyopata mgao mkubwa zaidi katika bajeti hiyo, ikitengewa Sh784.5 bilioni.
Kati ya fedha hizo, Tume ya Huduma kwa Walimu (TSC) itapata Sh424.3 bilioni kwa usimamizi wa walimu, Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu (HELB) Sh56.7 bilioni, elimu ya bure ya sekondari Sh54.6 bilioni na ufadhili wa Sekondari Msingi Sh30.7 bilioni.
Mbadi alisema karibu wanafunzi 500,000 wa vyuo vikuu tayari wamenufaika na ufadhili wa masomo na mikopo kupitia mfumo mpya wa ufadhili unaozingatia mahitaji na uwezo wa mwanafunzi.
Zaidi ya hayo, Sh30.9 bilioni zimetengwa kwa ufadhili wa wanafunzi wa vyuo vikuu huku Sh9.2 bilioni zikielekezwa kwa wanafunzi wa TVET.
Serikali pia imetenga Sh4.9 bilioni kuwaajiri walimu vibarua kazi za kudumu na Sh8.2 bilioni kusaidia walimu hao wakati wa mafunzo.
Mbadi alisema mageuzi ya elimu yamesababisha kuajiriwa kwa walimu 100,000 na kujengwa kwa zaidi ya madarasa 23,000 pamoja na kuanzishwa kwa maabara 1,600 ili kuimarisha utekelezaji wa mtaala mpya wa CBC.
Usajili katika vyuo vya kiufundi pia umeongezeka kutoka wanafunzi 562,499 mwaka 2022 hadi 825,484 mwaka 2025, hatua inayolenga kuzalisha ujuzi unaohitajika katika soko la ajira.