• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 8:55 PM
Warwanda wawili wakamatwa UG wakiendesha ujasusi

Warwanda wawili wakamatwa UG wakiendesha ujasusi

Na DAILY MONITOR

MAAFISA wa usalama wa Uganda wamekamata wanajeshi wawili wa Rwanda kwa madai ya kuingia nchini humo kukusanya taarifa za kijasusi.

Kukamatwa kwa wawili hao; Ishimwe Bosose na Peter Sanvura huenda kukazidisha kuzorota kwa uhusiano baina ya mataifa hayo jirani ambayo yamekuwa na uhasama kwa miezi kadhaa sasa.

Wanajeshi hao walikamatwa wakiwa kanisani katika eneo la Kamwezi wilayani Rukiga wikendi iliyopita.

Akizungumza alipopokea mwili wa Mnyarwanda aliyeuawa kwa risasi nchini Uganda karibu na mpaka wikendi iliyopita, meya wa wilaya ya Nyagatare nchini Rwanda, Claudian Mushabe, jana aliitaka serikali ya Rwanda kuachilia mara moja wanajeshi hao wawili.

“Tunashukuru serikali ya Uganda kwa kutuletea mwili wa raia wetu aliyeaga dunia akiwa huko. Vivyo hivyo, nasihi Uganda kuachilia huru watu wetu wanaozuiliwa huko,” akasema Mushabe.

Bw Mushabe hata hivyo, alikanusha madai kwamba watu waliokamatwa walikuwa wanajeshi.

Aliitaka serikali ya Uganda kuthibitisha madai kwamba Wanyarwanda waliokamatwa ni wanajeshi waliotumwa kukusanya taarifa za kijasusi.

Serikali ya Uganda imeshikilia kuwa wawili hao ni wanajeshi wa Rwanda ambao wamekuwa wakikusanya taarifa za kijasusi na wamepelekwa jijini Kampala ili wahojiwe.

Uhasama baina ya mataifa hayo jirani ulianza mnamo Februari, mwaka huu, Rwanda ilipofunga mpaka wa Katuna na kuonya raia wake dhidi ya kuzuru Uganda.

Rwanda ilidai kuwa Uganda inashirikiana na ‘maadui’ kutatiza serikali ya Rais Paul Kagame.

Mnamo Mei 17, waziri wa Mashauri ya Kigeni wa Uganda Sam Kutesa aliambia mabalozi wa mataifa mbalimbali kuwa wanajeshi wa Uganda wamekuwa wakiingia nchini Uganda bila ruhusa.

“Maafisa wa usalama wa Rwanda wamekuwa wakiingia nchini Uganda bila kufuata utaratibu uliopo,” akasema Bw Kutesa.

Unyanyasaji

Waziri wa Mashauri wa Kigeni wa Rwanda Richard Sezibera, mnamo Aprili pia aliambia mabalozi wa nchi mbalimbali kuwa Uganda imekuwa ikinyanyasa raia wake na hata kufadhili ‘magaidi’ ambao ni tishio kwa serikali ya Rais Kagame.

Wakati wa hafla ya kumwapisha kiongozi wa Afrika Kusini Cyril Ramaphosa, Jumamosi, Rais Kagame na kiongozi wa Uganda Rais Yoweri Museveni waliketi pamoja.

Huku wakiwa uwanjani Loftus Versfeld jijini Pretoria viongozi hao walionekana wakizungumza, katika hatua ambayo wadadisi walisema kuwa ilikuwa hatua muhimu katika kumaliza uhasama kati yao.

Jumatatu, mamia ya raia wa Uganda na mabalozi wa mataifa mbalimbali walikusanyika katika mpaka wa Katuna kushuhudia Uganda ikikabidhi Rwanda maiti ya mfanyabiashara John Batista Kyerengye aliyepigwa risasi na maafisa wa usalama wa Rwanda.

You can share this post!

Wanajeshi saba Gambia jela miaka tisa kwa kujaribu kupindua...

SHANGAZI AKUJIBU: Hajanitenda ila kuna wakati nashuku penzi...

adminleo