• Nairobi
  • Last Updated March 19th, 2024 2:13 PM
Kaunti kusambazia wakazi wa vitongojini maji

Kaunti kusambazia wakazi wa vitongojini maji

Na WINNIE ATIENO

SERIKALI ya Kaunti ya Mombasa imeanza kuweka mikakati kusambaza maji vitongojini ili kuimarisha afya za wakazi wa maeneo hayo.

Wakazi wa vitongoji duni wamekuwa wakikabiliana na hali ngumu ya maisha hasa ukosefu wa maji safi ya kunywa na hata kupikia.

Hali hii huwasababishia kuwa katika hatari ya maambukizi ya magonjwa hatari kama kipindupindu, kuendesha na hata kuumwa na tumbo.

Waziri wa kaunti anayesimamia maji na usafi Bw Tawfiq Balala amesema ufukara unachangia pakubwa hali hiyo.

“Ndiyo maana tumeanza kuweka mikakati kuimarisha maisha ya wasiojiweza katika vitongoji duni waweze kupata maji safi ili kuepuka magonjwa,” alisema Bw Balala.

Ametaja mitaa ya Muroto iliyoko Tudor kisiwani Mombasa kuwa mojawapo ya sehemu zinazolengwa sababu wakazi hawana maji safi.

Amesema wakazi hao wakipata maji safi wataepuka maradhi ambayo mara nyingi watoto ndio huwa hatarini zaidi.

“Wakazi wakipata maji, wanaweza kujiendeleza kifamilia na kibiashara na hata kupata mapato bora kuimarisha maisha yao lakini swala muhimu zaidi ni wakazi wapate maji safi, ” amesema Bw Balala.

Naibu Gavana wa Mombasa Dkt William Kingi amesema serikali ya kaunti inaendelea kuhakikisha wakazi wanapata maji wakati huu ambapo ulimwengu unakabiliana na janga la corona.

You can share this post!

Washukiwa watano wa mauaji ya polisi wakamatwa Lamu

Hatima ya Waiguru ni seneti lakini yeye afika mahakamani...

adminleo