• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 5:50 AM
TAHARIRI: Majaribio ya kuiba mitihani yazimwe

TAHARIRI: Majaribio ya kuiba mitihani yazimwe

Na MHARIRI

HABARI za hivi majuzi kwamba mikakati kabambe imewekwa kuiba mtihani wa kitaifa kwa shule za upili(KCSE) zinatamausha mno na ni sharti serikali iingilie kusitisha mpango huo.

Imefichuka kwamba baadhi ya wakuu wa shule za sekondari wanashirikiana na baadhi ya wazazi kukusanya hela za kununua karatasi za mtihani wa KCSE wa mwaka huu.

Baada ya mianya ya kuziba wizi wa mitihani kuwekwa, wahuni sasa wanaingilia mifumo ya ulinzi wa shule ili kufanikisha wizi huo.

Mpango wa wizi wa mitihani ni mkubwa mno na ni sharti serikali iwekeze pakubwa iwapo inataka kutangua shughuli hiyo inayoweza kuzamisha ndoto za watoto milioni 1.7 ambao watafanya mtihani huo mwezi Oktoba.

Ni hatia kubwa iwapo wanafunzi nao watafahamu kuhusu mpango huu wa wizi wa mitihani na kuendelea kushirikiana na wahuni hao na wasifanye lolote.

Mwaka 2017, Mwenyekiti wa Baraza la Mitihani(KNEC) Bw George Magoha alidokeza kuwa wahuni wanafanya juhudi kuhakikisha kwamba mtihani wa KCSE 2018 unafichuliwa mapema.

Wizi wa mitihani uliripotiwa mwaka jana baada ya jaribio la kufungua masanduku yaliyotumiwa kubeba karatasi za mitihani kabla ya kuanza kufanywa.

Huku maandalizi ya mitihani yakiendelea , ikiwa imesalia miezi mitano tu, KNEC yapaswa kuchukua hatua madhubuti kuzuia wizi huo.

Yapaswa kuwa zaidi ya kuwaita maafisa wakuu katika wizara ya elimu, Tume ya Kuajiri Walimu TSC na wakurugenzi wa elimu katika kaunti kujadili maandalizi ya mitihani ya kitaifa. Mkutano huo utafanyika Mei 31 katika Taasisi ya Ukuzaji Mitaala (KICD), Nairobi.

Prof Magoha alionya kuhusu mikakati hiyo ya wizi wa mitihani lakini pia akatahadharisha kuhusu adhabu kwa watakaopatikana.

Haijalishi kwamba walimu wamefanya juhudi zote kuwaandaa wanafunzi kufanya KCSE halafu matokeo yao yakataliwe kutokana na wizi wa kura. Huu ni ufisadi wa hali ya juu na ndio maana jinamizi hilo linaendelea kuzonga nchi.

Mbali na matokeo yao kukataliwa, wale wanaopenya kuingia vyuoni wanakuwa mbumbumbu hawawezi kumudu masomo ya chuo kikuu yanayohitaji kiwango cha juu cha kisomo. Hatimaye tunapata marubani ambao hawaifahamu kazi yao barabara, madaktari wasiomudu udaktari nk. Wizi wa mitihani ukomeshwe!

Ni tovuti ya Gazeti la Kampuni ya Nation Media Group
Mkurugenzi Mkuu: STEPHEN GITAGAMA
Mhariri Mkuu: TOM MSHINDI
Mhariri : PETER NGARE

You can share this post!

Demu ararulia polo long’i akisaka hela

Wajumbe mbioni kuhakikisha Trump na Kim Jong-Un wamekutana

adminleo