Bambika

Kukimbilia maisha kuliniangusha, Ray C sasa aungama

Na SINDA MATIKO July 19th, 2024 1 min read

RAY C staa wa bongo flava aliyewahi kuvuruga chati za burudani Tanzania amedai kuwa, sababu zake za kupoteza dira kwenye sanaa zilichangiwa pakubwa na ma-ex wake kipindi kile nyota yake ya muziki ilikuwa inang’aa.

“Kipindi kile nilikuwa mdogo halafu nimezungukwa na watu wengi sikuwa najua nani mzuri nani mbaya. Halafu nilikuwa mdogo na kupenda kuwa na watu. Mimi kudeti na watu ambao sikuwajua vizuri pamoja na kupenda kuwa na watu ndio jambo lililoniangusha. Walioniangusha ni wale watu wangu niliowaweka karibu iwe ni mpenzi wangu au marafiki. Niliowakaribisha kwa moyo mmoja ndio walioniponza mimi,” Ray C kafunguka.

Staa huyo ameongeza kwamba kutokana na hamu ya kula ujana, hakuwa anakataa jambo.

“Sikuwa mtu wa kusema hapana, pili niliwaamini watu sana, nikiambiwa kunywa Tequilla ndio huyo mimi, nikiambiwa kunywa Malaika shots ndio huyo mimi hujui yamewekwa nini na mwisho wa siku yakanikuta. Nilikuwa mdogo nimechangamkia maisha, nina pesa na jina lipo. Kilichoniponza ni mimi kuwa na kiherehere cha kutaka kujua kila kitu, niliparamia.”

Ray C ametoa kauli hiyo akiwahamasisha mademu wa Gen Z akitaka wawe makini na kasi za maisha ambayo anasema anaziona kwa kizazi cha 2000, kasi ambayo anakiri ilimponza.

“Hawa watoto wa 2000 wana kasi na ndio iliyoniponza. Nilikuwa na kiherehere cha kutaka kujua kila kitu ndio naona watoto hawa wakiwa nayo.”