Huruma yatoweka mtaa wa Huruma uliokusudiwa kuwa kimbilio la wengi
RISASI iliyomuua mwanafunzi wa KMTC, Cherly Adhiambo, katika mtaa wa Huruma, Nairobi, Jumamosi iliyopita haikuua tu maisha, ilipasua pia utulivu dhaifu wa kitongoji kilichozoea majanga yanayojitokeza bila onyo.
Mlio huo mmoja wa risasi uliweka wazi mizani hatari kati ya utulivu na vurugu inayotambulisha Huruma, mtaa uliobuniwa kuwa kimbilio lakini sasa umenaswa katika mgogoro uliokusudiwa kuepuka.
Huruma, jina linalomaanisha huruma, ulianza kama makazi ya familia zilizoondolewa maeneo mengine ya jiji la Nairobi lilipokuwa likipanuka.
Kwa muda, mpango huo ulifaulu. Lakini baada ya miongo kadhaa, huruma imezidi kupungua.
Mojawapo ya alama zinazoshtua zaidi ni safu ya majeneza yanayoonyeshwa kando ya Barabara ya Juja, kuanzia karibu na Kituo cha Polisi cha Huruma hadi makutano ya Kanisa la Redeemed Gospel, umbali wa takriban kilomita moja.
Majeneza hayo ni ukumbusho wa kimya wa jinsi maisha na mauti yanavyoishi bega kwa bega.
Huruma, iliyoko kati ya mitaa ya Kiamaiko na Ngei, iko urefu wa takriban kilomita moja na nusu kutoka Barabara ya Juja hadi Mto Nairobi.
Ni eneo lenye msongamano mkubwa wa watu na wakazi wake wanasisitiza kuwa kwa kiasi kikubwa ni tulivu. Hata hivyo, kwa wageni, Huruma mara nyingi huchukuliwa kama eneo la vurugu.
Steve Macharia, mkazi wa muda mrefu na mwenyekiti wa Chama cha Wakazi wa Huruma Flats, ameshuhudia ukuaji wa mtaa huo tangu mwishoni mwa miaka ya 1970.
Anasema msongamano wa watu ndio chanzo kikuu cha changamoto zake.
“Miundombinu iliwahi kuwa ya kutosha. Maji yalikuwepo, mfumo wa majitaka ulifanya kazi na hakukuwa na taka nyingi,” anasema.
Hali hiyo sasa imebadilika, huku majaa ya taka yakiwa kila mahali na kuhatarisha afya ya watoto.
Idadi ya wakazi wa Huruma haijarekodiwa rasmi, lakini kama eneo la kipato cha chini, lina msongamano mkubwa na makazi yanayokosa mpangilio.
Miaka ya 1980 hakukuwa na majengo ya ghorofa nyingi.
Kufikia miaka ya 1990, majengo ya ghorofa tatu yalijengwa. Leo, mengine yanafikia ghorofa saba, yakizidi uwezo wa huduma zilizopo.
Awali, Huruma ilikuwa na nyumba za serikali, zikafuatwa na shule. Karibu na kingo za mto, makazi yaliyojengwa kiholela yaliibuka, yakileta ukosefu wa usalama, usafi duni na msongamano.
Kando ya Barabara ya Juja, Cosmas Masika anaendesha karakana ya useremala ya Imani Furniture tangu ahamie hapa kutoka Gikomba mwaka 2012.
“Hapa ni mahali pazuri kwa sababu ya shughuli nyingi,” anasema.
Karibu naye ni Humphrey Shikoli Anyole, mmoja wa mafundi wanaotengeneza majeneza yanayoonekana barabarani. Anasema licha ya maandamano kugeuza eneo hilo kuwa hatari mara kwa mara, majeneza huguswa kwa nadra.
“Watu wanaogopa kuyaingilia kwa sababu ya utamaduni wa kuheshimu wafu,” anasema.
Ndani zaidi ya makazi, makazi yamejengwa karibu na mto ambako mifumo ya maji taka na mifereji ni duni. Wakazi wanaishi kwa ukaribu mkubwa, hali inayowasaidia kutambua wageni kwa haraka na kudhibiti uhalifu.
“Ikiwa mtu anajulikana kuwa mhalifu, tunamwita mbele ya chifu na kumwonya,” anasema Bw Macharia.
“Asipobadilika, tunashirikisha wenye nyumba na kumtaka aondoke.”
Hata hivyo, wakazi wanasema malalamishi yao kuhusu uhalifu, majengo haramu, taa duni na kuchelewa kwa polisi mara nyingi hayazingatiwi hadi janga litokee.
“Huu ni mtaa mzuri,” anasema Auma, aliyeomba atambulike kwa jina moja kwa hofu ya kulengwa.
“Lakini tunaishi kwa hofu ya usalama. Tumewaajiri walinzi wa kibinafsi na bado haitoshi. Njia za waenda kwa miguu na maegesho yamevamiwa na wachuuzi. Laiti Huruma ingekuwa kama ilivyokusudiwa.”
Takriban miaka 50 tangu kuanzishwa kwake, Huruma bado imening’inia kati ya matumaini na uhalisia—ikikabiliana ana kwa ana na mgogoro iliokusudiwa kuepuka.